Yanga wapata winga mpya wa ukweli




BAADA ya mshambuliaji mpya wa Yanga,Geofrey Mwashiuya kufanya mazoezi ya wiki moja na kikosi hicho, kocha Hans Pluijm amefunguka na kutamka ni mchezaji wa ukweli na atamchezesha winga ya kushoto.
Lakini Mwashiuya akatoboa siri nzito kwa kusema, alikataa pesa za Simba, Azam zilizokuwa zinamwania hapo awali na kusaini Yanga kwa sababu alikuwa anaipenda tangu utotoni.
Pluijm aliliambia Mwanaspoti: “Nimemwangalia mazoezini naweza kusema ni mchezaji mzuri ambaye ana kila kitu. Ni kijana mdogo ambaye anatakiwa apewe muda na atakuja kuisaidia vizuri Yanga hapo baadaye kikubwa ajitambue.”
“Na kutokana na staili yeke, nitamtumia kucheza winga ya kushoto, hapo ndipo mahali pake,”alisema Pluijm. Kwa upande wa Mwashiuya ambaye alisajiliwa na Yanga kwa mkataba wa miaka mitatu akitokea Kimondo ya Mbozi mapema mwaka jana alisema: “Sifichi, niliamua kuja kuichezea Yanga kwa sababu ya mapenzi. Naipenda Yanga tangu nilipokuwa mtoto mdogo.”
“Na siku nilipopigiwa simu kuwa wananihitaji, nilifurahi sana, kwani kama siyo mapenzi, ningeweza kusaini Simba au Azam hapo awali, walinifuata nisaini kwao,”alisema Mwashiuya.
Akizungumzia ushindani ndani ya kikosi hicho, Mwashiuya alisema: “Ushindani upo mkubwa, mimi ni mgeni kwenye timu nahitaji muda, lakini ninachoahidi ni kuwapa raha ile wanayoitaka mashabiki na wapenzi wa klabu hii, kikubwa wanipe muda.”
Mwashiuya ametua Yanga ambako atawania namba na mawinga wengine kama, Mrisho Ngassa, Simon Msuva, Mbrazil Andrey Coutinho na Nizar Kharfan.
Kwa upande wa Pluijm alisema: “Mwashiuya ni kijana mdogo, lakini ni mchezaji ambaye amekamilika kwa kila kitu na uhakika akiendelea hivi, ataisaidia timu hapo baadaye.”
“Kutokana na staili yake, kama kocha nitamtumia kucheza winga ya kushoto,”alisema Pluijm.

No comments