Yanga haikamatiki
AFRIKA Mashariki jana kulikuwa na mechi mbili kubwa kwenye Ligi
za ndani, Kenya
kulikuwa na mpambano wa Mashemeji baina ya Gor Mahia na AFC Leopards ambao uliisha kwa sare ya bao 1-1. Lakini kimbembe kilikuwa Bongo, Yanga ilizidisha kiburi na jeuri kwa kuthibitisha kwamba msimu huu haikamatiki kotekote baada ya kuifumua Mbeya City mabao 3-1 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
kulikuwa na mpambano wa Mashemeji baina ya Gor Mahia na AFC Leopards ambao uliisha kwa sare ya bao 1-1. Lakini kimbembe kilikuwa Bongo, Yanga ilizidisha kiburi na jeuri kwa kuthibitisha kwamba msimu huu haikamatiki kotekote baada ya kuifumua Mbeya City mabao 3-1 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Yanga imeendeleza jeuri hiyo ikiwa ni siku chache
baada ya kuinyuka Coastal Union mabao 8-0 huku ikiwa na kumbukumbu nzuri
kimataifa baada ya kuipiga chini Platinum ya Zimbabwe na sasa inapiga
kifua ikimaanisha Etoile du Sahel waje hata sasa hivi.
Vinara hao wa Ligi Kuu wamebakiza pointi tano tu
kukata tiketi ya kucheza michuano ya CAF mwakani na pointi 11 kuwavua
Azam ubingwa baada ya ushindi wao wa jana.
Ushindi huo umeifanya Yanga kufikisha pointi 46,
nane zaidi ya ilizonazo Azam yenye pointi 38 baada ya juzi
kung’ang’aniwa tena na sare dhidi ya Mtibwa Sugar ikiwa ni mara ya pili
mfululizo.
Pointi hizo zinaifanya Yanga kubakisha pointi tano
ili kupata moja ya nafasi mbili za uwakilishi wa Tanzania katika
michuano ya kimataifa na kuwafungia njia Simba wenye pointi 35 na
inayoweza kufikisha pointi 50 tu ikishinda mechi zake zote.
Pia Yanga imebakiza pointi 11 tu kuweza kuwavua
Azam ubingwa kwani itafikisha pointi 57 ambazo haziwezi kufikiwa na
watetezi hao hata wakishinda mechi zao zote kwani itaweza kufikisha
pointi 56 tu.
Katika pambano hilo lililochezeshwa vema na
mwamuzi Mathew Akram, Yanga ilianza kwa kasi dakika tano za kwanza kwa
kulishambulia lango la wapinzani wao na dakika ya sita Amissi Tambwe
aliandika bao, lakini lilikataliwa kwani kabla ya kufunga mwamuzi wa
pembeni alinyoosha kibendera.
Hata hivyo walisahihisha makosa katika dakika ya
18 baada ya Kpah Sherman kufunga bao la kwanza akimalizia shuti
lililotemwa la Haruna Niyonzima. Hilo likiwa bao la pili kwa Mliberia
huyo msimu huu.
Vijana wa Hans vand der Pluijm waliendelea
kuliandama lango la wapinzani wao na kufanikiwa kuandika bao la pili
katika dakika ya 37 kupitia kwa Salum Telela aliyefunga kwa shuti kali
baada ya kuanzishwa mpira wa adhabu na Niyonzima.
Mbeya City waliotoka kuwabana Azam kwa kutoka nao
sare ya 1-1 Jumatano iliyopita ilicharuka na kupata bao lao dakika tano
kabla ya mapumziko kupitia kwa Themi Felix ‘Mnyama’ baada ya kuwafunga
tela mabeki wa Yanga kabla ya kupiga ‘chop’ iliyoshindwa kudakwa na kipa
Ali Mustafa.
Kipindi cha pili kilianza kwa kasi na Mbeya City
kukosa mabao ya wazi kabla ya kuruhusu bao katika dakika ya 49 baada ya
nahodha Nadir Haroub ‘Cannavaro’ kuunganisha kwa kichwa mpira wa adhabu
ya Niyonzima. Mbeya ilipata pigo dakika nne baadaye baada ya Themi
kulimwa kadi nyekundu na mwamuzi Mathew Akrama baada ya kumchezea
madhambi Salum Telela. Telela alijikuta akishindwa kuendelea na mchezo
huo na kutolewa nje na nafasi yake kuchukuliwa na Hassan Dilunga. Licha
ya kucheza pungufu, Mbeya City waliibana Yanga na hasa baada ya kufanya
mabadiliko ya wachezaji kwa kuwatoa Deus Kaseke, Raphael Alpha na Paul
Nonga na kuwaingiza Peter Michael, Mwegane Yeya na Abdallah Seif.
YANGA: Ally Mustafa ‘Barthez’, Juma Abdul, Oscar
Joshua, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kelvin Yondani, Mbuyi Twite, Salum
Telela/Hassan Dilunga, Haruna Niyonzima, Amissi Tambwe, Kpah
Sherman/Mrisho Ngassa na Simon Msuva.
Post a Comment