Hesabu zaibeba Simba nafasi ya pili




KOCHA wa Simba, Goran Kopunovic amesema hesabu zinaibeba timu hiyo katika mbio za kuwania nafasi ya pili ambapo amezitaja mechi mbili dhidi ya Mbeya City na ile na Azam kuwa ndiyo zimeshikilia tiketi yao ya kupanda ndege.
Azam imeonekana kutetereka katika mechi mbili zilizopita baada ya kutoa sare na Mbeya City na kisha Mtibwa hivyo kusalia katika nafasi ya pili na pointi 38 baada ya kucheza mechi 20 wakati Simba inashika nafasi ya tatu na pointi 35 baada ya mechi 21.
Kopunovic ambaye timu yake iliifunga Toto Africa mabao 3-0 katika mchezo wa kirafiki juzi Jumamosi jijini Mwanza, alisema sasa timu yake imerejea rasmi katika mbio za nafasi ya pili.
Hata hivyo alisema wanatakiwa kushinda mechi zote tano kama wanahitaji nafasi hiyo.
Hesabu zipo hivi; Sasa Simba inatakiwa kuiombea njaa Azam ipoteze mechi mbili halafu Simba iibuke na ushindi katika mechi baina yao ili Azam ishindwe kufikisha pointi 49 ambazo Simba itafikisha kama itashinda michezo yote hiyo.
Endapo Azam itafanikiwa kushinda michezo mitatu na kupata sare moja katika michezo yake sita iliyosalia itakuwa imeiondosha Simba rasmi katika mbio za nafasi hiyo ya pili kwani watafikisha pointi 49 ambapo pia timu hiyo ina wastani mzuri wa mabao ya kufunga na kufungwa.
Hata hivyo rekodi zinaonekana kuibeba Azam kwani katika mechi nne za mwisho zilizozikutanisha timu hizo, Azam imeshinda mara mbili na nyingine mbili zilimalizika kwa sare.

 


No comments