Simba yafanya kweli, Ukawa watoa msimamo. Hii ni habari kamili

 
SIMBA imezidi kuongeza presha kwa Azam baada ya jana kupata ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Kagera Sugar katika pambano la kiporo uliochezwa kwenye uwanja wa Kambarage, Shinyanga.



Ushindi huo umeifanya Simba kupunguza pengo la pointi baina yake na Azam kutoka nne hadi kuwa moja, kwani imefikisha pointi 35 baada ya mechi 21, wakati watetezi hao wa Ligi Kuu wanaoshuka uwanjani kesho kucheza na Mbeya City wana pointi 36 kutokana na mechi 18.
Mabao ya Simba katika mechi hiyo ya jana iliyokuwa imelazwa toka Jumamosi kutokana na mvua yaliwekwa kimiani kupitia kwa Ramadhani ‘Messi’ Singano aliyefunga kwa shuti kali dakika ya 49 kabla ya Rashid Mandawa kusawazisha bao dakika ya 60 akimalizia krosi ya Adam Kingwande.
Bao hilo limemfanya Mandawa kumkamata Didier Kavumbagu wa Azam katika ufungaji akiwa na bao 10.
Hata hivyo Simba ilijihakikishia ushindi katika dakika ya 65 baada ya kupata penalti baada ya mabeki wa Kagera kuunawa mpira na Ibrahim Ajibu kutumbukiza kiufundi mkwaju huo na kusaidia timu yake kupata pointi tatu muhimu na kuwazima Kagera waliotamba kabla ya mchezo huo.
SIMBA UKAWA 
Mashabiki wa Tawi la Mpira na Maendeleo maarufu Simba Ukawa, wamesema kuwa kundi lao kamwe haliwezi kufa kutokana na vifo vya wenzao vilivyotokea Ijumaa kwa ajali ya gari kwani lina zaidi ya wanachama 100 wenye uwezo mkubwa wa kuendeleza kundi hilo.
Katika ajili hiyo ya barabarani iliyotokea eneo la Makunganya, Morogoro, ilisababisha vifo vya wanachama saba wa tawi hilo akiwemo katibu wao Mohamed Kingolile ‘Ngumi Jiwe’ na jana Jumatatu walimazia kumzika mwanachama wao Rashid Baltazar aliyezikwa Yombo Dovya, Dar es Salaam.
Mweka Hazina ambaye pia ni mratibu wa safari za Ukawa, Jaffari Mussa, aliliambia Mwanaspoti kuwa msiba waliopata ni mkubwa ila hauwezi kuwazuia kuishangilia Simba katika mechi zao zozote na hawawezi kuvunja kundi hilo.
Mratibu huyo pia alikemea vitendo vya baadhi ya mashabiki wa Simba aliodai wanaeneza sumu kwa viongozi kuwa vitendo hivyo haviisaidii Simba kimaendeleo na vinaleta migogoro.
“Tumepatwa na msiba huu viongozi wa Simba wamekuja waliwakilishwa na Makamu wa Rais, Geofrey Nyange ‘Kaburu’ aliyekuja mpaka Morogoro hospitali, lakini kuna wanaojichanganya na sisi walitaka kumfanyia fujo kwa kumfukuza, huo si utu wala uungwana.
Majeruhi watano kati ya 24 waliojeruhiwa katika ajali hiyo watalazimika kuchunguzwa zaidi afya zao na madaktari bingwa. Mganga mfawidhi wa hospitali ya rufaa mkoa wa Morogoro, Dk Ritha Lyamuya alithibitisha hilo.

No comments