Waarabu waishtukia Yanga, Simba watia mkono Dar






Etoile ambao ni wadeni wa Simba, watacheza na Yanga kwenye raundi ya pili ya michuano ya Kombe Shirikisho baada ya kuiondoa Benfica de Luanda ya Angola kwa mabao 2-1

YANGA ikishinda mechi nne zijazo kwenye Kombe la Shirikisho itanukia utajiri, lakini Kocha wa Etoile de Sahel, Faouzi Benzarti na mkurugenzi wake wa michezo, Zied Jaziri wameshtukia ishu kwamba wanaweza kuumbuka wasipojipanga.
Etoile ambao ni wadeni wa Simba, watacheza na Yanga kwenye raundi ya pili ya michuano ya Kombe Shirikisho baada ya kuiondoa Benfica de Luanda ya Angola kwa mabao 2-1.
Yanga ambayo itacheza mechi ya kwanza Aprili 18 kwenye Uwanja wa Taifa itarudiana ugenini wiki mbili baadaye kisha ikivuka itachezwa droo kwa kuchanganya na timu zilizotolewa kwenye raundi ya pili ya Ligi ya Mabingwa ambapo zitachezwa mechi mbili kusaka wa kuingia hatua ya makundi ya Shirikisho ambako ndiko kwenye mkwanja.
Vigogo wa Etoile wameonyesha kushtushwa na ufanisi wa timu hiyo haswa kwa kuangalia kasi ya Yanga na kwamba wameamua kujipanga upya kila idara tayari kwa lolote linaloweza kutokea huku wakisisitiza kwamba wanaanza mashindano na Yanga.
Yanga ikifanikiwa kushinda mechi nne zilizosalia na kutinga hatua ya makundi hata wakienda kuchemsha huko wana uhakika wa noti kwani timu itakayokuwa ya mwisho kabisa kwenye kundi ina uhakika wa Sh 270milioni pamoja na kuuza wachezaji wake, lakini ikikomaa ikiwa angalau ya tatu itapata Sh432milioni.
Jaziri alisema jana kwamba licha ya joto kali na changamoto walizokumbana nazo Angola wamevuka kutokana na kujituma na juhudi za timu.
“Tunahitaji kuiangalia zaidi mechi ijayo (dhidi ya Yanga) kwavile ndiyo itakayoamua mbio za ubingwa kwenye haya mashindano,”alisema Jaziri.
Kocha Benzarti kwa upande wake alisema hakuna mechi rahisi kwenye michuano hiyo ya Afrika ndio maana walijitahidi kupata bao la mapema ili kumaliza mchezo dhidi ya Benfica na sasa wameelekeza nguvu kwenye mechi na Yanga ili kuhakikisha wanarejesha hadhi ya klabu hiyo.
Makamu wa Rais wa Etoile, Dr. Jalel Krifa alisema: “Tumetimiza lengo moja kwa kuingia kwenye hatua nyingine muhimu bila kuwa na majeruhi, tutapambana kwa jitihada zaidi katika mchezo unaofuata kwavile ni muhimu zaidi kuliko huku tulikotoka.” Kiongozi huyo aliongeza pia kwamba wana mzigo mkubwa kwenye mechi za Ligi Kuu ya Tunisia hivyo wanahitaji kujipanga.
SIMBA WATIA MKONO
Simba inaidai Etoile du Sahel ya Tunisia Dola 300,000 zaidi ya Sh 500 milioni ikiwa ni deni la fedha za mshambuliaji wao Emmanuel Okwi alipouzwa kwenye klabu hiyo ambapo viongozi wa klabu hiyo wamesema watajadili jinsi ya kulipwa fedha hizo.
Mwishoni mwa mwaka jana, Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa) liliitaka Etoile kuilipa Simba fedha hizo baada ya Simba kuishitaki kwa kushindwa kuwalipa kwa muda waliokubaliana lakini mpaka sasa Watunisia hao hawajafanya lolote kwa Simba.

                              Next

No comments