Simba hatarini kumpoteza straika huyu machachari



SIMBA inaweza kumpoteza mshambuliaji wake Mkenya, Raphael Kiongera, baada ya kushindwa kumlipa mshahara wake wa mwezi Desemba na Januari na amesema kwamba anasubiri wafikishe miezi mitatu ili achukue uamuzi mgumu.
Kiongera ambaye kwa sasa anafanya mazoezi na timu yake ya zamani KCB na ataichezea kwa mkopo wa miezi mitano, aliliambia Mwanaspoti kuwa mkataba wake upo wazi kwamba asipolipwa mshahara miezi mitatu, basi mkataba huo utakuwa umevunjwa.
Alisema ni mara nyingi amekuwa akiwapigia simu viongozi wake juu ya kuwakumbusha mishahara yake lakini wamekuwa wakimpa ahadi zisizotekelezeka.
“Unajua kwa sasa siwapigii simu tena, nimechoka kuzungushwa ila ninachokifanya ni kusubiri miezi mitatu ipite ili nichukue uamuzi wangu kwani watakuwa wamevunja mkataba wenyewe, haya ni maisha na mimi nategemea kuishi kupitia mpira, sasa wasiponilipa mshahara wanategemea naishije?” alihoji.
“Tulikubaliana kuanza kuichezea Simba msimu ujao ingawa daktari aliniambia naweza kuanza kucheza mwezi huu, wao walimsajili mchezaji mwingine lakini leo hii wanashindwa kunilipa mshahara wangu, wanataka niwabembeleze, ngoja nione mwisho wake ni nini.”
Kiongera alifanyiwa upasuaji wa goti mwaka jana nchini India na Simba ndio waliotoa gharama zote za matibabu kwa mshambuliaji huo, kwa kutumia Sh15 milioni.
Usajili wake Simba ulikuwa ni wa Dola 20 (Sh34 milioni) kwa miaka miwili na ameichezea Simba mechi moja tu ya ufunguzi dhidi ya Coastal Union waliyotoka sare ya bao 2-2.
Kwa mujibu wa makubaliano ya pande zote mbili, Kiongera ataanza kuichezea Simba msimu ujao wa ligi na sasa atacheza kwa mkopo KCB kulinda kipaji chake.
Imeelezwa beki Joseph Owino ndiye atakayetemwa katika usajili wa msimu ujao na nafasi yake itachukuliwa na Kiongera. Owino atakuwa amemaliza mkataba wake.
Hata hivyo, viongozi wa Simba walipoulizwa juu ya suala la straika huyo, hawakutoa ushirikiano.

No comments