Yanga ni kimataifa zaidi.. Hawa ndio watakaoivaa BDF XI ya Botswana Jumapili




WAWAKILISHI wa Tanzania katika Kombe la Shirikisho, Yanga, wamewafunika vibaya wapinzani wao katika michuano hiyo, BDF XI ya Botswana katika takwimu.
Kwa kuangalia takwimu hizo ni wazi kwamba miamba hiyo ya Jangwani inaweza kufanikiwa kuwaondosha DBF na kusonga mbele kwenye michuano hiyo.
Rekodi za BDF kwenye ligi ya Botswana msimu huu zinaonyesha timu hiyo inashika nafasi ya tatu na pointi 37 wakiwa wamecheza mechi 19 wakati Yanga wao wanaongoza Ligi Kuu Bara wakiwa na pointi 25 baada ya kucheza mechi 13.
BDF wamefungwa mabao 20 msimu huu ikiwa ni wastani wa bao moja katika kila mechi jambo linaloashiria kuwa wanafungika kirahisi wakati Yanga wao wamefungwa mabao saba pekee ikiwa ni wastani wa bao moja kwa mechi mbili jambo linaloleta matumaini ya ushindi kwa Yanga.
Yanga pia imepoteza mechi mbili pekee msimu huu wakati BDF wao wamefungwa mechi sita. Mabingwa hao wa mwaka 2013 wameonekana kuwa kwenye fomu zaidi wakiwa hawajapoteza mchezo wowote katika mechi sita za mwisho kwa kushinda mechi nne kati ya sita za mwisho za ligi na kutoka sare mbili wakati DBF wao wamefungwa mechi moja na kushinda tano katika mechi zake sita za mwisho.
Kocha wa Yanga, Hans Van Plujim alisema mechi hiyo ya kimataifa ni ngumu kwa Yanga lakini ushindi walioupata juzi Jumapili dhidi ya Mtibwa umepandisha morali yao na kuwapa nafasi kubwa ya kuibuka na ushindi.
“Unapokwenda kucheza mechi kubwa kama hiyo ya BDF na timu yako imetoka kushinda ni jambo zuri, morali ya wachezaji inakuwa juu na kila mtu anakuwa na ari ya ushindi, haitakuwa kazi rahisi lakini,” alisema.
“Bado hatujapata nafasi ya kuwaona wapinzani wetu, lakini tutafanya maandalizi ya kutosha kwa muda wa wiki nzima ili kujiweka pazuri, ni lazima tushinde mchezo huo wa kwanza na kuwaondoa katika mchezo wa pili ili tuweze kusonga mbele.”
Yanga itakuwa mwenyeji wa BDF Jumapili.

No comments