Kopunovic akataa kuitoa Simba



KOCHA Mkuu wa Simba, Goran Kopunovic, amepanga kesho Jumatano kikosi chake kitangulie mkoani Morogoro kuwafuata Polisi ya huko lakini ametamka kwamba kama kuna anayedhani Simba imejiondoa katika mbio za kuwania taji la Ligi Kuu Bara huyo anajidanganya.
Akizungumza na Mwanaspoti, Kopunovic alisema amepata taarifa kwamba baadhi ya mashabiki wameiondoa Simba katika mbio za ubingwa ambapo ametamka kwamba ni makosa makubwa kufikiria hilo.
Alisema kutokana na msimamo wa Ligi pamoja na mechi zilizosalia, bado Simba ina nafasi ya kugombea nafasi mbili za juu kwani mazingira wanayokutana nayo bado Yanga na Azam waliopo juu wanaweza kukutana nayo.
Alisema bado ana imani na kikosi chake na kwa sasa wanataka kusaka ushindi kwa staili ya kuangalia mechi zao huku wakisubiri wanaoongoza ligi kukumbana na mazingira magumu katika mechi zao.
“Mimi naangalia mambo kwa tofauti na wanavyofanya wengine, angalia mechi zilizosalia kwa timu zote utagundua kwamba yoyote anaweza kufanya makosa kama ambavyo Simba tumefanya,” alisema Kopunovic.
“Siku zote naiandaa Simba kushinda lakini kupata sare haya ni matokeo ya mpira, mazingira kama haya yanaweza kuzikumba timu zozote zilizopo juu yetu, tunachofanya sasa ni kujiandaa kwa mechi zetu tukisubiri kuona nini kitatokea kwa wapinzani wetu.”

No comments