Mrwanda anywa maji ya kishirikina
MASTRAIKA wawili wa Yanga wamekumbana na uchawi wa aina yake.
Kpah Sherman ambaye ni Mliberia amedai kuyabaini maji ya ushirikina
yaliyokuwa uwanjani, lakini mwenzake Danny Mrwanda akayachukua akayanywa
huku kipa aliyeyaweka akiwashangaa.
Kpah ambaye si mzungumzaji sana, alifichua tukio
hilo lililotokea kwenye mechi yao ya Ligi Kuu Bara dhidi ya Ndanda
kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam ambapo timu hizo hazikufungana.
Lakini mlinda mlango wa Ndanda, Wilbert Mweta,
ambaye ni kipa wa zamani wa Simba, aliposikia maneno ya Sherman
akashangaa. Katika mchezo huo, washambuliaji wa Yanga; Sherman, Mrwanda
na Simon Msuva walikosa mabao ya wazi wakiwa peke yao mbele ya lango,
kila walipopiga mipira ilipaa na kutoka nje hali ambayo iliwashangaza
wapenzi wa soka na mashabiki waliofika uwanjani hapo. Hata hivyo kocha
wa Yanga, Hans Pluijm, amepuuza madai hayo na kusema ni uzembe tu wa
wachezaji wake.
Sherman ameiambia Mwanaspoti kwamba kwenye goli la
Ndanda kulikuwa na maji ya ushirikina na aliyatoa kwa mikono yake baada
ya kugundua kwamba kipa huyo aliyanyunyizia kwenye goli na baadaye
akayabakiza mengine na kuyaweka pembeni ya mlingoti wa lango.
Baada ya Mliberia huyo kuyatoa maji hayo na
kuyatupa nje, bado yalikuwa magumu kwao kisha Mrwanda aliyafuata na
kuyanywa. Hata hivyo haikusaidia chochote kwani ndio kwanza wapinzani
wao walizidi kukaba huku wakijiangusha kupoteza muda.
Sherman aliiambia Mwanaspoti akisema: “Mimi ni
Mwafrika moja kwa moja naamini maji yale yaliwekwa vitu tu vya
kishirikina ikawa sababu ya kutukosesha mabao, ndiyo maana niliamua
kuyatupa nje, haiwezekani mtu na goli unapaisha.
“Pia nilimwona kwa macho yangu yule kipa, yale
maji aliyamimina (anaonyesha kwa ishara) kuanzia mwanzo wa goli hadi
mwishoni kwa nini alifanya vile ndio yalikuwa kikwazo kwetu,”alisema
Sherman ambaye Yanga wanamchukulia kuwa ndiye straika namba moja wa timu
yao.
Ingawa Mrwanda hakupenda kufafanua hilo, kipa
Mweta alijitetea akisema: “Ule ni mpira ndiyo maana tunafanya mazoezi,
hakuna ushirikina wala nini.
“Nimeshangaa sana kuona mchezaji mkubwa kama yule
kuamini mambo hayo ya kishirikina badala ya kucheza mpira, anajua
kiwango chake ni kidogo?”
Kocha Pluijm alisema hawezi kuwalaumu
washambuliaji wake kutokana na kitendo cha kushindwa kufunga mabao na
badala yake anaulaumu mfumo wa makuzi ya soka waliyokulia wachezaji hao
tangu utoto wao.
Pluijm alisema suala la kufunga ndiyo jambo kubwa
alilokuwa akiwaelekeza katika kipindi chote cha mazoezi yao na walikuwa
wanafanya vizuri mazoezi. Alisema aligundua tatizo hilo katika michezo
waliyocheza na Polisi Morogoro na Ruvu Shooting.
“Hatufungi, sina wasiwasi na safu ya ulinzi lakini
kwa washambuliaji tatizo lao ni ufungaji, nimekuwa nikilifanyia kazi
kwa siku zote kwenye mazoezi yetu na wachezaji walikuwa wanafanya
vizuri,” alisema kocha huyo.
Post a Comment