Sserunkuma athibitisha




KWA kipindi kirefu mashabiki wa Simba walianza kupoteza imani na mshambuliaji wao Mganda Dan Sserunkuma kutokana na kushindwa kwake kuzifumania nyavu.
Baadhi ya mashabiki na hata wanachama wa Simba katika kutapatapa na matatizo yaliyokuwa yakiikabili timu yao, walianza kumnyooshea kidole mshambuliaji huyo na kumuona si mwenye msaada katika timu.
Fikra na mtazamo huo umekuja kutokana na imani kubwa waliyokuwa nayo mashabiki hao kwa mshambuliaji huyo ambaye alikuwa moto wa kuotea mbali wakati akiichezea Gor Mahia ya Kenya.
Kwa kuwa akiwa na Gor Mahia aliibuka Mfungaji Bora wa Ligi Kuu Kenya, baadhi ya mashabiki waliamini kasi hiyo ya mabao ingeendelea katika Ligi Kuu ya Tanzania Bara na kwamba mshambuliaji huyo angeanza moja kwa moja kwa kufunga.
Baada ya kuona matarajio yao hayatimii wakaanza kupoteza imani naye na kujenga hisia kwamba klabu yao imesajili mchezaji mzigo na wengine kuja na dhana kwamba hajitumi na hivyo Simba haihitaji kuendelea kuwa naye.
Matokeo mabaya ya kufungwa na Mbeya City mabao 2-1 ndiyo yaliyoongeza hasira za mashabiki wa Simba na katika kusaka mchawi, Sserunkuma naye akaingizwa katika kundi hilo hilo la wachezaji wasio na msaada Simba.
Hata hivyo wapo japo wachache waliojenga imani kwamba mshambuliaji huyo alihitaji muda wa kuzoea mambo mengi yakiwamo mazingira na hata uchezaji wa timu kwa ujumla.
Na pengine imani hiyo ya wachache imeanza kuthibitika katika mechi ya juzi ya Ligi Kuu Bara ambako Simba iliibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya JKT Ruvu, mechi iliyopigwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. 
Kilichoanza kumkuta Sserunkuma kinatukumbusha mambo ya kukatishana tamaa katika soka la Tanzania.
Cha kufurahisha ni kwamba uongozi wa Simba hakukuwa tayari kumezwa na hisia za kwamba Sserunkuma ni mzigo.
Uvumilivu ambao umeonyeshwa na viongozi hasa makocha wake ndilo jambo ambalo linatakiwa kufuatwa na viongozi na hata mashabiki wa klabu nyingine. Ni kweli kwamba kila shabiki wa Simba alipenda kumuona mchezaji huyo akiendeleza kasi yake upachikaji mabao kama ilivyokuwa wakati akiwa nchini Uganda.
Na hata timu pinzani kwa kuzingatia rekodi ya mchezaji huyo pengine waliamini kwamba angekuwa na madhara makubwa kwa timu zao.

No comments