Zengwe jingine laibuka ndani ya Yanga..




YANGA imeibua zengwe jipya ambalo huenda likaidhohofisha timu ya Polisi Morogoro ambayo usajili wake wote  hauzidi Sh40 milioni. Pesa hizo ni thamani ya straika mmoja wa Yanga, Kpah Sherman.
Polisi Morogoro, ambayo haijawahi kushinda mchezo tangu straika wake, Danny Mrwanda aende Yanga, inacheza na Yanga mjini Morogoro kesho Jumamosi kwenye mechi ya Ligi Kuu na  Yanga imeamua kuiibulia zengwe ambalo huenda likatibua mipango yao kama litafanikiwa.
Yanga imesisitiza kwamba straika Said Bahanuzi iliyemtoa kwa mkopo Polisi Morogoro haruhusiwi kucheza dhidi yao Jumamosi na akichezeshwa wanalianzisha. Bahanuzi ndiye straika aliyefunga bao moja na pekee la Polisi kwenye mechi tatu mfululizo. Polisi baada ya kuondokewa na Mrwanda imecheza mechi tatu, ikasuluhu mbili dhidi ya Stand na Coastal pamoja na sare ya bao 1-1 na Ndanda.
Lakini Polisi wamesisitiza kwamba ni lazima Bahanuzi acheze kwani walikubaliana kuhusu jambo hilo tangu anasaini. Katibu wa Polisi, Leus Yazidi, aliliambia Mwanaspoti kuwa walikubaliana na Yanga wamtumie katika mechi zote za Ligi Kuu hata dhidi yao hadi atakapomaliza mkopo wake wa miezi sita katika klabu hiyo inayomilikiwa na Jeshi la Polisi.
“Unauliza kuhusu Bahanuzi? Ndiyo, tutamtumia katika mechi yetu na Yanga kwani ni moja kati ya vitu tulivyokubaliana wakati tunamsajili kwa mkopo kutoka kwao. Tutamtumia, na  sasa tunamuandaa ili atupatie ushindi dhidi ya timu yake ya zamani,” alisema Yazidi.
Wakati Polisi ikiamini hivyo, Katibu wa Yanga,  Jonas Tibohora alisema Polisi haiwezi kumtumia Bahanuzi katika mchezo dhidi yao kwani kanuni zilizopo ni kwamba mchezaji anayecheza kwa mkopo timu nyingine haruhusiwi kucheza dhidi ya timu yake labda kuwe na makubaliano maalumu ya maandishi.
“Bahanuzi hawezi kucheza dhidi yetu, ndivyo kanuni zinavyosema sasa kama wao wanasema watamtumia sawa tutaona nani mshindi katika kanuni, wala hatuna tatizo,” alisema Tibohora ingawa kwenye kanuni za uhamisho wa wachezaji wa Ligi Kuu Bara hakuna kipengele kinachosema mchezaji asicheze dhidi ya timu iliyomkopesha.
Kwa upande wake, Bahanuzi alisema amejipanga vilivyo kuwatoa nishai mabeki wa Yanga, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kelvin Yondani na Mbuyu Twite kwani anawajia kivingine na wajiandae.
“Nipo kazini sitajali kwamba Yanga nimeitumikia miaka miwili nitakachoangalia ni jinsi gani nazitikisa nyavu zao naomba tu ushirikiano kutoka kwa wachezaji wenzangu kwani mabeki wao nawajua jinsi walivyo, nimejifunza mbinu mpya tangu nilipotua Polisi Moro nikiongeza na za kwangu naamini nitaisumbua safu ya ulinzi ya Yanga, nimejipanga naomba uzima kwa siku hiyo,”alisisitiza mchezaji huyo, ambaye haogopi zengwe la Yanga.

No comments