Sserunkuma ni moto kwa sasa




STRAIKA wa Simba, Elius Maguli amesema ameshafahamu aina ya uchezaji wa straika mwenzake, Danny Sserunkuma na wakiendelea kucheza pamoja wanaweza kufunga mabao zaidi.
Maguli na Sserunkuma wote waliifungia Simba ilipoilaza Ndanda mabao 2-0 wikiendi iliyopita na kufufua matumaini ya safu ya ushambuliaji ya timu hiyo iliyoshindwa kufunga mabao mengi katika michuano ya Kombe la Mapinduzi iliyomalizika punde huko visiwani Zanzibar.
Maguli alisema awali alipata tabu kufahamu aina ya uchezaji ya Sserunkuma lakini kwa kadiri siku zinavyozidi kwenda wamekuwa wakizoeana na huenda wakafanya makubwa zaidi siku zijazo.
“Nashukuru kwa sasa tumeanza kufanya vizuri, kama unavyojua Danny (Sserunkuma) alikuja wakati timu imebadili kocha, haikuwa kazi rahisi kwa kocha mpya kujua namna ya kutuchezesha kwa pamoja.
“Tumeendelea kufanya kazi katika mazoezi ya timu kuhakikisha tunazidi kuelewana ili tuweze kufunga zaidi, siyo kazi rahisi lakini tunapambana,” alisema Maguli, ambaye alifunga mabao 14 akiwa Ruvu Shooting msimu uliopita.
“Mwanzoni pia kufunga ilikuwa kazi ngumu kwasababu timu ilikuwa haifanyi vizuri, ile hali ilitusumbua sana kwani morali ya timu ilishuka na kila wakati tukawa tunajihisi wanyonge.”
Wakati huohuo, katika mazoezi ya Simba juzi Jumanne jioni kwenye Uwanja wa Boko Veterani, Sserunkuma alishindwa kutamba kwenye zoezi la ufungaji baada ya mashuti yake sita aliyopiga kushindwa kulenga goli na mengine kuokolewa na makipa akimwacha, Emmanuel Okwi raia wa Uganda aking’ara.
Pamoja na hayo, Kocha wa Simba, Goran Kopunovic alisema: “Kiujumla sina wasiwasi kabisa na kiwango cha Sserunkuma katika timu yangu.
Namwamini na ndiyo maana nimekuwa namtumia kila wakati. Sserunkuma ni mchezaji mzuri sijui hapo awali, lakini sasa kadri ya siku zinavyozidi ubora wake umekuwa unaongezeka, anajiamini na kufanya maamuzi sahihi, nafikiri hapo awali, woga na ugeni ndivyo vilivyokuwa vinamsumbua,”alisema Kopunovic.
Simba inajiandaa na mechi yao ya ligi watakayocheza keshokutwa Jumamosi katika Uwanja wa Taifa dhidi ya Azam FC.

No comments