Yanga yatoa onyo kwa TFF kuhusu haya...
HAPA kazi ipo. Yanga imevumilia na kuamua
kutoa onyo kwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) juu ya vitendo vya
kibabe wanavyofanyiwa wachezaji wake katika mechi zake.
Timu kubwa za soka nchini,
Simba, Yanga na sasa Azam FC, zimekuwa zikikumbana na vitendo vya kibabe
na udhalilishaji kwa nyota wake hasa wanapocheza na timu nyingine za
Ligi Kuu bara na kukaa kimya.
Lakini Yanga imeamua kuweka wazi
kukerwa na tabia hizo baada ya wachezaji wake akiwemo straika Amissi
Tambwe kuchezewa kibabe na mabeki wa Ruvu Shooting wikiendi iliyopita
kwenye Uwanja wa Taifa.
Tambwe amesimulia mateso
anayoyapata kutoka kwa mabeki wa timu pinzani katika mechi za ligi hiyo
na kuwataja wawili ambao ni vinara kwa kazi hiyo kila anapokutana nao
uwanjani.
Lakini wakati Tambwe
akilalamikia undava anaochezewa, mojawapo ya timu alizokumbana nazo,
Ruvu Shooting imeibuka na kusema: “Hana lolote ameshindwa kuhimili
muziki wetu.”
Akizungumza na Mwanaspoti Tambwe
ambaye ni raia wa Burundi alisema katika maisha yake ya soka nchini
amekuwa akikutana na mateso makubwa kutoka kwa mabeki watatu ambao
wamekuwa wakimfanyia vitendo visivyofaa vinavyoambatana na
udhalilishaji.
Tambwe alisema beki wa kwanza
katika kazi hiyo ni George Osei ambaye amekuwa akimfanyia vitendo hivyo
ikiwemo kumkaba vibaya katika kila mchezo. Osei sasa anachezea Ruvu
Shooting ambayo wikiendi iliyopita ilitoka suluhu na Yanga.
Alisema mabeki wengine ni Sunza
Shaaban maarufu kwa jina la Chogo ambaye sasa anachezea Mwadui ya
Shinyanga, lakini alikuwa anakumbana naye wakati anacheza Ruvu pia, wa
mwisho ni Michael Aidan wa timu hiyo hiyo.
“Hao mabeki wamekuwa wakinitesa
sana, sina maana kwamba sitaki kukabwa lakini ni wazi hawastahili
kucheza soka kwa njia wanazofanya, hawanitendei haki hata kidogo. Hawa
wanakukaba huku wakikuambia maneno mbalimbali yasiyofaa mara wewe
mkimbizi, hivi wanajua vita kweli hawa? Mimi naijua vita wasithubutu
kumwambia mtu mkimbizi,” alisema Tambwe.
“Kuna huyu Aidan nimeambiwa na
wenzangu aliwahi kuitwa hata timu ya taifa ya Tanzania lakini kuna mambo
ambayo anayafanya ipo siku ataisababishia Tanzania madhara makubwa kama
atachezeshwa, hawa wanatakiwa kufungiwa ili wajifunze.”
Awali Mkuu wa Idara ya
Mawasiliano ya Yanga, Jerry Muro alisema uongozi wao umesikitishwa na
matukio ya Tambwe kunyanyaswa na kupigwa uwanjani ambapo jana
waliwasilisha malalamiko yao kwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) huku
wakiorodhesha mapendekezo yao matano.
Muro alisema wanaitaka TFF
kuwachukulia hatua kali wahusika wote waliobainishwa kufanya vitendo
hivyo huku wakitaka ripoti ya mchezo huo kuwekwa hadharani kubaini
mapungufu ya waamuzi.
Post a Comment