Yametimia.. habari kutoka AFCON. Soma kila kitu hapa



MIKIKIMIKIKI ya fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (Afcon 2015) itaanza kutimua vumbi leo Jumamosi kwa wenyeji Guinea ya Ikweta kukipiga na Congo kabla ya Burkina Faso kukwaruzana na Gabon.
Kesho Jumapili michuano hiyo itaendelea kwa Mabingwa wa Afrika 2012, Zambia kushuka uwanjani kuchuana na DR Congo, kabla ya Tunisia kucheza na Cape Verde.
Fainali hizo za 30 zitaanza kwa matumaini ya mashabiki kupata uhondo na burudani bab’kubwa ya mchezo wa soka licha ya kukumbwa na changamoto nyingi ikiwamo hofu ya maradhi ya Ebola.
Awali fainali hizo zilitarajiwa kufanyika Morocco, lakini nchi hiyo ilijitoa na Shirikisho la Soka Afrika (CAF) kupeleka uwenyeji wa michuano hiyo katika nchi ya Equatorial Guinea.
Mechi za michuano hiyo zitafanyika katika miji minne mikubwa, Bata, Malabo, Mongomo na Ebebiyin ambako viwanja vingi vipya vilivyojengwa kwa ajili ya fainali hizo bado havijakamilika vizuri, huku uwanja uliopo Ebebiyin umeripotiwa kuwa na uwezo wa kuingiza mashabiki 5,000 tu.
Mwaka 2012 uwanja huo uliweka rekodi baada ya mashabiki 200 tu kwenda kutazama mechi hizo.
Kutokana na mwamko mdogo wa mashabiki kwenda uwanjani kutazama mechi jambo hilo limemfanya rais wa nchi hiyo, Teodoro Obiang Nguema kununua tiketi 40,000 kwa ajili ya kuzigawa kwa mashabiki ili wajitokeze kwenye michezo hiyo.
Ebola yatishia usalama
Virusi vya maradhi ya ugonjwa huo vilianza kusambaa maeneo ya Afrika Magharibi Machi, mwaka jana na kusababisha vifo vya watu 8,386 katika nchi sita tofauti hadi kufikia Januari 12, mwaka huu.
Uwepo wa maradhi hayo unatishia hali ya usalama wa kiafya na jambo ambalo linaweza kutibua zaidi fainali hizo zikashuhudiwa na mashabiki wachache.
Hata hivyo, kwa nchi ya Equatorial Guinea hakuna mgonjwa wa Ebola iliyewahi kuripotiwa kutokea katika ardhi hiyo baada ya kuajiri madaktari wataalamu wa kueneza elimu ya kuepuka maambukizi.
Kwenye ukanda huo wa Afrika Magharibi nchi zilizoathirika zaidi ni Guinea, Sierra Leone na Liberia na kwamba wachezaji wote wanaokwenda kwenye fainali hizo walifanyiwa vipimo kuona kama kuna mwenye virusi hivyo vya maradhi hayo hatari. Timu inayopewa nafasi ya kushinda taji ni Algeria.

No comments