Wachezaji hawa ni tishio kwa mkwanja msimu ujao..
Licha ya makosa yake madogo
madogo na ubinafsi uwanjani, bado Msuva anabaki kuwa moja ya nguzo
muhimu katika kikosi cha Yanga. Hakuna mtu mwenye wasiwasi na uwezo
wake.
Licha ya ubora wake huo, Msuva
hawezi kupiga pesa yoyote pale Yanga kwa sasa. Alisaini mkataba mpya
kabla ya kuanza kwa msimu na atalazimika kusubiri kwa mwaka mmoja zaidi
ili aweze kupata mkataba mpya. Maisha hayajamtendea haki. Yanga pia
haina mpango wa kumuuza kwenda timu nyingine.
Ukiachana na Msuva, wapo mastaa
kadhaa ambao wamefanikiwa kupandisha thamani zao na wanatarajiwa kupiga
pesa za maana mwishoni mwa msimu. Mwanaspoti inakuletea orodha ya mastaa
hao;
Didier Kavumbagu, Azam FC
Straika Mrundi, Didier Kavumbagu
anajiamini na anaamini katika kile anachokifanya uwanjani. Kavumbagu
alijiunga na Azam mwanzoni mwa msimu huu baada ya kumaliza mkataba wake
na Yanga. Licha ya kuachwa Yanga baada ya mkataba wake, Kavumbagu
alisaini mkataba wa mwaka mmoja pekee pale Azam na hakuwa na papara ya
kutaka mkataba wa muda mrefu. Aliamini katika kazi yake na kile
anachokwenda kukifanya uwanjani. Wachezaji wengi wanaogopa mikataba hiyo
mifupi kwa hofu ya kushuka viwango na kutemwa mwisho wa msimu lakini
kwa Kavumbagu ni tofauti. Tayari ameifungia Azam mabao saba katika mechi
10 za Ligi Kuu Bara na kuiwezesha timu hiyo kujikita kileleni mwa
msimamo wa ligi na pointi 20. Kwa sasa straika huyo anasubiri msimu
umalizike apige pesa za maana katika mkataba mpya.
Ame Ally, Mtibwa
Straika wa Mtibwa Sugar, Ame
Ally ni miongoni mwa wachezaji waliotarajiwa kupiga pesa za maana
katika dirisha dogo la usajili mwezi uliopita, lakini mambo yalikwenda
ndivyo sivyo na kuendelea kubaki katika kikosi cha timu hiyo. Ame
ameonyesha uwezo mkubwa wa kufunga mabao kwani katika mechi saba za
awali za ligi alikuwa amefunga mabao manne. Baada ya mafanikio hayo Ame
ameendelea kutulia na maisha ya Mtibwa na tayari amefunga bao lake la
tano katika mechi tisa alizocheza. Mzaliwa huyo wa Zanzibar hana papara
na anaonekana kukomaa na kazi yake ya upachikaji wa mabao ili aweze
kuzivutia timu nyingi zaidi mwisho wa msimu. Ame anatajwa kuwa miongoni
mwa mastaa watakaopiga mkwanja wa maana mwisho wa msimu.
Rashid Mandawa, Kagera
Straika wa Kagera Sugar, Rashid
Mandawa huenda akafuata nyayo za mastaa kadhaa waliopita klabuni hapo
kama Mrisho Ngassa, Amri Kiemba na Themi Felix kwa kuchota fedha za
maana katika usajili wa mwisho wa msimu. Straika huyo ameonekana kuwa
moto msimu huu akiwa amefunga mabao matano katika mechi 10 alizoichezea
Kagera. Mandawa pia alifanikiwa kutwaa tuzo ya Mchezaji Bora wa Novemba
na kuwapiku mastaa kadhaa wanaoshiriki ligi hiyo. Utulivu wake uwanjani,
mwili wake wenye nguvu na uwezo wake wa kumiliki mpira huenda ukazitoa
udenda timu kadhaa za ligi kuu na kumsajili kwa dau la maana mwisho wa
msimu.
Post a Comment