Tambwe apagawishwa Yanga, hajui cha kufanya.. Pata habari kamili





AMISSI Tambwe amepagawa na viwango vinavyoonyeshwa na mastraika wenzake katika kikosi cha Yanga na amekiri wanampa wakati mgumu wa kujua afanye nini cha ziada ili kujihakikishia namba kikosi cha kwanza.
Mrundi huyo ameliambia Mwanaspoti kuwa anashangazwa na uwezo unaoonyeshwa na wenzake hasa Mliberia Kpah Sherman na wazawa; Danny Mrwanda na Jerry Tegete, anaosema wamekuwa na mazoezi ya hali ya juu siku chache tangu watolewe katika Kombe la Mapinduzi.
Alisema: “Mastraika wenzangu wananipa changamoto kubwa kikosini, wanafanya vizuri kila siku hivyo wananipa wakati mgumu kumshawishi kocha kuwa mimi ndiye straika bora kuliko wao. Sijui nifanye nini ili kuweza kuwa juu yao.
“Najua natakiwa kujituma zaidi, lakini mchuano ni mkali na kama kocha akiamua kumtumia mmoja wetu tu kikosini hapo, hali ndiyo itakuwa mbaya zaidi, tuna ushidani mkali hata mazoezini.”
Tambwe ambaye alisajiliwa Yanga Desemba mwaka jana baada ya kutemwa na Simba, alisema tofauti na timu nyingine, mastraika kikosini hapo kila mmoja ni mpambanaji na ana uchu wa kufunga kuanzia mazoezini hadi kwenye mechi.
“Wote kuanzia Sherman, Mrwanda na Tegete wanacheza soka la hali ya juu. Nina uhakika kocha atakuwa anaumiza akili yupi wa kumpanga na yupi wa kumweka nje, hakika hapa natakiwa kufanya kazi ya ziada vinginevyo mambo yatakuwa magumu,” alisema.
“Lakini ushindani huu unatufanya tuwe na timu imara, siyo siri timu itakayokutana na sisi tutaiangushia kipigo kikubwa.”
Jumamosi Tambwe anaweza kuichezea Yanga dhidi ya Ruvu Shooting katika mwendelezo wa Ligi Kuu Bara kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Msimu uliopita Tambwe alipoichezea Simba dhidi ya Ruvu, alifunga mabao mawili timu yake ikishinda 3-2. Yanga iliifunga Ruvu mabao 7-0.

No comments