Hiki ndicho kinachowaleta Mabosi wa Arsenal Tanzania




KLABU ya Arsenal imepanga kutuma maofisa biashara wake jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kujadili fursa za ushirikiano na wafanyabiashara kadhaa wakubwa wa nchini.
Huu utakuwa ujumbe wa kwanza kabisa wa Arsenal nchini Tanzania ambapo klabu hii kubwa ya Ligi Kuu England inataka kujenga ushirika katika maeneo ya masoko na chapa zake, ili kutanua mafanikio yaliyofikiwa kwenye nchi nyingine za Afrika zikiwamo Kenya, Uganda na Nigeria.
Arsenal inataka kutoa fursa kwa benki za Tanzania pamoja na kampuni za simu na taasisi nyingine kuweza kupata rasilimali zihusianazo na klabu hiyo ya London, kama vile bidhaa zilizosainiwa kwa majina ya wachezaji na tiketi za mechi zao za soka.
Ofisa Biashara Mkuu wa Arsenal, Vinai Venkatesham, alisema wameichagua Tanzania kwa sababu wana washabiki wengi na kwa kushirikiana na taasisi za hapa, watakuwa karibu zaidi na mashabiki wao kuliko ilivyokuwa awali.
“Katika bara lenye nchi zaidi ya 50, tumechagua kuzuru Tanzania kimkakati kwa sababu tunaiamini nchi hii,” alisema.
“Arsenal ina mamilioni ya Watanzania ambao ni washabiki waaminifu na wenye mapenzi makubwa nayo, hivyo kwa kushirikiana na taasisi za hapa, tutaweza kuisogeza klabu karibu zaidi na mashabiki.”
Wajumbe hao wa jopo la Maendeleo ya Ushirikiano ya Arsenal wanatarajia kuwasili nchini Januari 18 na kukaa kwa wiki moja jijini Dar es Salaam, wakiitisha mikutano kadhaa na wafanyabiashara.
Ujio wa viongozi wa timu hiyo umeratibiwa na kampuni ya EAG Group Tanzania ambapo Ofisa Mtendaji Mkuu wake, Imani Kajula alisema: “Ujio huu utainufaisha zaidi Tanzania kukua katika sekta mbalimbali.”

No comments