Ngassa atoroka Yanga




YANGA imetenga Sh168 milioni kwa ajili ya mechi mbili za awali za Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya BDF XI ya Botswana itakayochezwa Februari 14, lakini Mrisho Ngassa ametorokea Afrika Kusini kufanya majaribio ya soka la kulipwa.
Ngassa ambaye amewahi kuzichezea Simba, Azam na Kagera Sugar, amekosekana katika timu hiyo kwa wiki moja sasa ambapo uongozi unaeleza kwamba anamuuguza ndugu yake ambaye maelezo yake hayajawekwa wazi.
Lakini Mwanaspoti lina habari kwamba mchezaji huyo aliyewahi kutakiwa na Westham ya England pamoja na El Merreikh ya Sudan, yupo Afrika Kusini akifanya majaribio na klabu ya Free State Stars ambayo imekuwa ikimfuatilia kwa kipindi kirefu na wakala mmoja tajiri nchini Tanzania ndiye aliyemuunganisha na timu hiyo.
Mtendaji Mkuu wa shughuli za kila siku za Yanga ambaye ni Katibu Mkuu, Jonas Tibohora, alisema Ngassa aliondoka akiomba ruhusa maalum ya kumuuguza ndugu yake, lakini uongozi kupitia vyanzo vyake umepata taarifa kwamba yuko Afrika Kusini akisaka timu ya kumsajili bila ya ruhusa.
Tibohora ambaye kitaaluma ni daktari wa Sayansi ya Michezo, alisema taarifa hizo wamezipata kutoka kwa baadhi ya wadau wa klabu yao ambao wamemuona mshambuliaji huyo nchini humo huku klabu inayotajwa kwamba ndiyo inataka kumsajili ni Free State Stars ambayo iliwahi kumfanyia majaribio mwaka jana.
Alisema kwa sasa wanaendelea na uchunguzi wa hilo akisema endapo watabaini ukweli katika utovu huo wa nidhamu wa mshambuliaji huyo, atakaporudi watakutana naye huku akidokeza uwezekano wa kuishitaki Free State Stars.
“Alikuja kwangu akaomba ruhusa kwamba anamuuguza ndugu yake, kibinadamu hatukuweza kumzuia tukamkubalia, lakini taarifa tulizopata ni kwamba hayuko nchini kitu ambacho kilitushtua na hata tulipokuwa tunamtafuta kutaka kujua maendeleo ya mgonjwa wake hatukuwa tunampata,”alisema Tibohora.
“Awali nilimshtukia Ngassa wakati anaomba ruhusa alitaka pia tumpatie barua ya kwenda kushughulikia pasi yake ya kusafiria, nilijiuliza kuna uhusiano gani kati ya mgonjwa na pasi ya kusafiria sikupata majibu tunaendelea na uchunguzi wa hilo,”alisisitiza kiongozi huyo ambaye klabu yake inakabiliwa na mechi mbili za Ligi Kuu Bara dhidi ya Ndanda na Mtibwa kabla ya kuingia kwenye michuano ya kimataifa.
YATENGA SH168 MILIONI
Habari za uhakika ambazo Mwanaspoti imezipata wikiendi iliyopita ni kwamba Yanga imetenga Sh168 milioni katika Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya BDF XI ya Botswana.
Yanga imepanga kutumia Sh36 milioni katika maandalizi ya mchezo wa kwanza dhidi ya BDF utakaochezwa nchini Februari 14 na itatumia dola 78,000 (Sh132 milioni) katika mchezo wa marudiano utakaochezwa Botswana wiki mbili baadaye.
Msimu uliopita wa Ligi ya Mabingwa Afrika, Yanga iliweka bajeti ya dola 78,000 pia ili kuivaa Al Ahly ya Misri katika mchezo wa marudiano uliochezwa Misri.Hata hivyo Yanga ilitolewa na Al Ahly kwa penalti 4-3 baada ya kufungwa bao 1-0 huku wakiwa wameshinda bao 1-0 nyumbani.

No comments