Hawa ni Mastaa wanne wa Yanga wanaohujumiwa..


Kocha wa Yanga, Hans Pluijm akiwa katika pozi kwenye mazezi

KOCHA wa Yanga, Hans Pluijm, amegundua hujuma za kuwafanyia rafu na kuwaumiza makusudi wachezaji wake wanne kwenye mechi za Ligi Kuu Bara na ameahidi kupambana nazo ingawa amewaonya waamuzi kuwa makini.
“Yanga kila mchezo inaocheza ni kama fainali, kunakuwa na vita kubwa kati ya wachezaji wangu na mabeki wa timu pinzani, sitaki kusema nataka wasikabwe lakini kuna tatizo katika namna ya kuwazuia wanaumizwa sana tena kwa makusudi kabisa,” alisema Pluijm.
“Timu yangu inaundwa na wachezaji wenye majina, hakuna timu inayotaka kufungwa, lakini tatizo ni jinsi wanavyokabiliana na wachezaji wangu. Marefa wawe makini zaidi katika kuangalia ni jinsi gani wanakabwa, ili kuepuka madhara,”anasisita Pluijm.
Wachezaji hao wanne ambao Pluijm amesema wanafanyiwa fujo na hujuma za waziwazi uwanjani huku waamuzi wakishuhudia ni Amissi Tambwe, Kpah Sherman na viungo wa pembeni Andrey Coutinho na Simon Msuva.
Ametamka kwamba wamekuwa wakiumizwa bila sababu za msingi na mabeki wasio waungwana wa timu pinzani jambo ambalo limekuwa likiathiri kasi ya Yanga ambao imesuka kikosi cha kutwaa kombe msimu huu.
Pluijm amesisitiza kwamba hataki timu yake ipendelewe na waamuzi, lakini akawaonya waamuzi hao kuhakikisha wanaongeza umakini kugundua rafu wanazochezewa washambuliaji wao ambao wamekuwa wakikamiwa vibaya na timu pinzani.
Katika hatua nyingine pia Mholanzi huyo amesisitiza kwamba Deo Munishi ‘Dida’ ndiye kipa namba moja nchini, lakini kinachomsikitisha wapo watu wanamkatisha tamaa badala ya kumpa moyo anapokosea.
Dida alikosa mechi yao ya Jumamosi dhidi ya Ruvu Shooting waliyotoa suluhu na Ally Mustapha ‘Bartez’ ndiye alidaka mchezo huo. Yote ni kutokana na madai kuwa ameshuka kiwango na hakufanya vizuri katika mechi zake za mwisho hasa walipocheza na Azam FC wakatoa sare ya mabao 2-2.
Akizungumza na Mwanaspoti, Pluijm alisema: “Napenda ushindi na mpira ni ushindi, lakini nakubali pia soka ni mchezo wa makosa. Yapo makosa yanaweza kutokea kwa binadamu yoyote bila kutegemea.”
“Mfano, binafsi naamini kuwa, Dida ni namba moja, anayefanya vizuri kwenye soka la Tanzania, lakini kuna mambo yanayofanyika kama kumkatisha tamaa jambo ambalo linaweza kumharibia, akapotea kabisa mchezoni,”alisema Pluijm.
“Yapo makosa na yanatokea hata Ulaya ipo hivyo kwa anayeangalia soka la huko anajua. Kama Dida alifanya makosa yanaweza kumtokea binadamu yoyote na kinachotakiwa kufanya ni kumpa moyo ili awe vizuri na arudi katika hali yake, lakini siyo kumkatisha tamaa, anaweza kupotea kabisa.”

No comments