Sserunkuma anena juu ya Kaseja

 
 

STRAIKA wa Simba, Dan Sserunkuma amesema kwamba kiwango alichofikia kipa Juma Kaseja alitakiwa kwenda kucheza soka la kulipwa na sio kujiunga Yanga baada ya kumalizika mkataba wake na Simba kwa kile alichoeleza kwamba uamuzi wake unammaliza kisoka.
Sserunkuma aliliambia Mwanaspoti katika mahojiano maalumu kuwa, Kaseja ni miongoni mwa wachezaji aliokuwa akiwasikia na alibahatika kumwona katika michuano ya Kombe la Challenji lakini ameshangazwa kuona sasa hivi hadaki japokuwa amesajiliwa na timu kubwa ya Yanga.
Alisema kuwa kwa sasa Kaseja siyo mchezaji tena wa kuzichezea timu hizi kongwe nchini Simba na Yanga na badala yake atafute timu nyingine nje ya nchi kama ilivyokuwa kwa kipa mwenzake, Ivo Mapnuda, ili kujijengea heshima.
“Kuna kipindi nilisikia kuna timu ya nje inamhitaji, kwa nini hakwenda huko? Unajua kwasasa hawezi kuonekana wa maana kwani timu anazozichezea ni zile zile Simba na Yanga, hawawezi kuona ubora wake, ni vyema angekwenda huko alikokuwa anahitajika kuliko kwenda Yanga.
“Kaseja baada ya kumaliza mkataba na Simba angeamua kwenda nje naamini angejenga heshima kubwa kama ilivyo kwa Ivo, alitoka hapa akaenda Gor Mahia alijenga kiwango na heshima ndio maana Simba wakamchukuwa tena, Kaseja si wa kukaa benchi,” alisema Sserunkuma.
Katika usajili wa dirisha dogo uliofungwa Desemba 15, Kaseja ambaye mwaka jana FC Lupopo ya Kongo DR walikuwa wanamuhitaji, alikuwa anatajwa kurudi Simba baada ya kuiandikia barua ya kusudio la kuvunja mkataba wake na Yanga kwa maelezo kwamba wamekiuka mkataba kwa kushindwa kummalizia fedha yake ya usajili Sh 20 milioni kati ya Sh 40 milioni walizokubaliana.
Hata hivyo, Yanga tayari wamemwandikia barua wakili wa Kaseja ambaye ni Kampuni ya Mbamba Advocate ya kutaka walipwe Sh 340 milioni ikiwa ni fidia ya usumbufu wa gharama za kuvunja mkataba pamoja na fedha ya usajili wake.

No comments