Sserunkuma huyu ni moto


 

USAJILI wa dirisha dogo kwa timu za Ligi Kuu Bara na Ligi Daraja la Kwanza ulifungwa Jumatatu ambapo baadhi ya timu zimeweza kusajili ili kuimarisha vikosi vyao, lakini nyingine hazijasajili kwa kuamini ubora wa vikosi vyao.
Kila timu inatakiwa kuwa na wachezaji 30, lakini timu nyingi katika usajili wa msimu huu hazikuweza kujaza nafasi zote ambapo sasa wamejaza nafasi hizo katika usajili wa dirisha dogo. Timu hizo ni pamoja na Simba ambayo imesajili wachezaji watatu wa kigeni ambao ni Dan Sserunkuma, Simon Sserunkuma na Juuko Murshid ambao wote ni raia wa Uganda. Dan na Simon hawana undugu wowote bali majina tu ndio yamefanana.
Usajili wa Dan Sserunkuma ndiyo ulionekana kutikisa katika timu hiyo ya Simba, ni kwa kuamini kwamba ni straika imara kutokana na rekodi yake ya Gor Mahia ambapo amekuwa Mfungaji Bora mara mbili mfululizo katika Ligi Ku Kenya (KPL), msimu wa 2012/13 na 2013/14.
Sserunkuma alicheza kwa kiwango cha juu na kuisadia Gor Mahia kwa kiasi kikubwa kutwaa ubingwa wa ligi hiyo msimu wa 2012/13 ambapo alifunga mabao 17 na kuwa Mfungaji Bora wa msimu huo na msimu wa 2013/14 alifunga mabao 16. Kwa muda aliokaa Gor Mahia amecheza mechi 73 na kufunga mabao 49 kwenye mashindano yote.
Sserunkuma alikuwa anahitajika na timu ya FC Banants ya Armenia inayoshiriki Ligi Kuu ya nchini humo lakini straika huyo aligoma kwenda kwani aliona Gor Mahia bado ni timu inayomfaa kwa wakati huo ingawa timu hiyo bado ilionyesha nia hata wakati Simba ikimuwania.
Pia, mwaka 2013, Sserunkuma alipata tuzo ya Mchezaji Bora iliyoandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Uganda (USPA) akiwapiku wachezaji wenzake; Tony Mawejje anayecheza Norway na Siraje Muhindo anayeichezea timu ya Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Mbarara (MUST).
Katika mahojiano na Mwanaspoti, straika huyo aliweza kuelezea mambo mbalimbali katika soka hasa nini atawafanyia wana Msimbazi hao katika mechi zilizobaki za ligi.
Nani amemleta Simba
“Hapa kuna rafiki zangu kama Emmanuel Okwi na Joseph Owino, viongozi wa Simba waliponihitaji niliwauliza kwanza hao jinsi maisha ya hapa yalivyo, kwani sikuwahi kuishi hapa zaidi ya kuja mara moja tulipocheza na Simba mechi ya kifariki.
“Hivyo nilivutiwa sana na jinsi walivyonieleza Okwi na Owino, niliona nije kujaribu kama nitaweza soka la hapa japo soka la Afrika Mashariki halina tofauti sana ingawa Kenya wapo makini katika soka lao na ndio maana wanatoka sana,” anasema.
“Baada ya kujiridhisha kutoka kwa Okwi na Owino, nilikuja hapa, tulizungumza na kukubaliana jinsi ya malipo na nililipwa, nilifanyiwa vipimo na kusaini siku hiyo hiyo, baada ya kumalizana nao nilirudi nyumbani kwa ajili ya kujipanga kuja kuichezea Simba rasmi.
“Niliridhika na fedha niliyopewa na ndio maana nilikubali kusaini mkataba na sikuona kama kuna sababu ya kwenda nchi nyingine ambako kuna timu zilikuwa zinanihitaji, nitakuwepo Simba mpaka nitakapomaliza mkataba wao kama nilivyoondoka Gor Mahia baada ya kumaliza mkataba,” anasema Sserunkuma.

No comments