Huu ndio mpango wa Pluijm


 

SASA mtaitambua Yanga. Imetangaza sekretarieti mpya iliyosheheni wasomi kwenye fani mbalimbali pamoja na kutambulisha benchi jipya la ufundi litakalokuwa chini ya Mholanzi Hans Pluijm ambaye naye amechimba mkwara wa maana.
Mwenyekiti wa Yanga, Yusuf Manji kupitia Mkuu mpya wa Idara ya Habari na Mawasiliano Jerry Muro ametangaza sekretarieti mpya itakayoongozwa na Katibu Mkuu, Jonas Tibohora. Omar Kaya amekabidhiwa idara ya Masoko, Sheria amepewa Frank Chacha huku fedha ikiongozwa na Baraka Deusdedit.
Ikaushie hiyo safu mpya. Pluijm alitangazwa kuchukua nafasi ya Mbrazil Marcio Maximo aliyesitishiwa mkataba wake na klabu hiyo alisema baada ya kuona ubora wa wachezaji wake wa zamani na wale wapya washambuliaji Amissi Tambwe raia wa Burundi, Mliberia Kpah Sherman na mzawa Danny Mrwanda kazi ya kuunda kikosi hicho itaanza rasmi leo Jumamosi.
Amesisitiza kwamba kurudi kwake Yanga anataka kurudisha nguvu ya soka la kushambulia litakaloambatana na nidhamu ya uwanjani na nje ya uwanja ambapo amewataka mashabiki wa timu kumpa siku saba tu afanye mambo yake na wamiminike kwenye Uwanja wa Taifa kuangalia mambo yake dhidi ya Azam FC watakaoumana nao Desemba 28.
“Nafurahi kuona kwamba kila mtu ndani ya Yanga anafurahia ujio wangu, nawaomba mashabiki wa Yanga na wanachama wenzangu watulie watuachie nafasi tuitengeneze timu mimi na msaidizi wangu Charles (Mkwasa),” alisema Pluijm ambaye Mwanaspoti linafahamu kwamba amesaini mktaba wa mwaka mmoja na nusu.
“Naijua Yanga, hii ni timu yangu, najua natakiwa kuanzia wapi kurudisha nguvu yake iliyopungua hivi karibuni, nataka kuwaona wachezaji wote kesho (leo) nasikia kuna wapya nataka kujua ubora wao baada ya hapo nitaanza kurudisha nguvu ya timu,”alisisitiza kocha huyo kwa kifupi huku akiwakumbushia mashabiki jinsi alivyoinoa Yanga iliyoitoa ulimi nje Al Ahly ya Misri kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika.
Habari kutoka ndani ya uongozi zinasema kwamba Pluijm ameona video za mechi za Yanga na kusema matokeo ya kutoridhisha ya timu hiyo yametokana na mambo mengi ikiwemo wachezaji kukosa ari ya kupambana.
Kwa mujibu wa kigogo mmoja wa Yanga, kocha huyo aliomba kuona vipande vya video hizo za mechi za Yanga na kugundua vitu kadhaa ambavyo viliigharimu timu. “Alipoona video hizo, ametuambia kuna vitu havipo sawa katika timu kwanza hiyo ari ya kupambana kwa wachezaji haipo kabisa kwani wachezaji wanakuwa kama hawana uchungu na timu na wanacheza huku wakikosa umakini,” alisema.
Katika hilo kocha huyo amewahakikishia atarejesha uwezo wa pumzi kwa wachezaji wote ili waweze kupambana kwa dakika zote uwanjani lakini kwa kucheza soka la kuonana na siyo kutegemea mipira mirefu pekee.
Bosi huyo amewaambia mabosi wake kwamba mabeki lazima wakabe kwa akili na kucheza soka la kuonana na siyo kuharakisha kupiga mipira mirefu kwani ni rahisi kwa adui kuinasa na kuweka chini kisha kuwamaliza.

No comments