Simba yamtisha Haruna Niyonzima



 
KIUNGO wa Yanga, Haruna Niyonzima, ameitazama Simba ya sasa na kusema wachezaji wake wengi wanacheza kwa kujiamini.
Niyonzima raia wa Rwanda, alisema tofauti na walivyocheza mechi za nyuma katika Ligi Kuu Bara, sasa wachezaji wengi wa Mnyama wanaonekana kubadilika na kucheza soka la kujiamini na wana uwezo wa kupambana kwa dakika zote.
“Simba wanajiamini sana sasa hivi na hii ni tofauti na walivyokuwa wakicheza mwanzo katika ligi, hawakuwa vile kama walivyocheza,” alisema.
“Kama wakitulia na kucheza vile kila siku, basi watakuwa na ushiriki mzuri katika ligi na kuweza kupata mafanikio. Hata hivyo na sisi Yanga hatupo vibaya sana kwani tuna timu nzuri ya ushindani ambayo inaweza kupambana na timu yoyote ile.”
Licha ya kuifunga Yanga mabao 2-0 wikiendi iliyopita katika mechi ya Nani Mtani Jembe, Simba ilipata ushindi mara moja tu katika mechi saba za ligi ilizocheza na kujikuta ipo nafasi ya saba ikiwa na pointi tisa.
Simba itacheza mechi yake nyingine ya ligi Desemba 26 dhidi ya Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Novemba Mosi mwaka jana Simba ilipocheza na Kagera Sugar kwenye uwanja huo, timu hizo zilitoka sare ya bao 1-1 na kutokea vurugu.

No comments