Simba yaikomoa yanga


Straika wa Yanga Amissi Tambwe (aliyevaa jezi nyekundu) akiitumikia timu yake ya zamani, Simba SC

UAMUZI wa Yanga kumsainisha straika, Amissi Tambwe unaiumiza Simba na uongozi umekiri kwamba Danny Serrunkuma wa Uganda bado hajaonyesha walichokipandia ndege na kumfuata Kenya kumnunua.
Habari za ndani zinadai kwamba Simba ambayo safu yake ya ushambuliaji bado haina mtu wa kati wa kuaminika, imekata tamaa ya kumrudisha Tambwe baada ya Yanga kumuahidi mkataba wa maana hivyo sasa ili kukata ngebe za wapinzani wao Mnyama ameamua kuingia msituni.
Kwahiyo? Simba wameanza mchakato rasmi wa kitaalamu kusaka straika atakayeikomoa Yanga uwanjani kwa vitendo na kuwasahaulisha mashabiki wa Msimbazi wasimkumbuke Tambwe. Uongozi pia umeridhika na kiwango cha kocha wao, Goran Kopunovic. Rais wa Simba, Evans Aveva ameitumia Mwanaspoti kuweka wazi kwamba Sserunkuma mwenye mabao matatu bado hajafanya walichokitarajia katika usajili wake ingawa hawajakata tamaa kwa kuwa anaendelea kuzoea mazingira ya Ligi Kuu Tanzania Bara.
Alisema wanajua kwamba Kopunovic anataka straika wa kati mwenye kujua kufunga ambapo tayari wameanza mchakato wa siri kusaka kifaa na pia wanaendelea kufuatilia uwezo wa mshambuliaji wao Raphael Kiongera ambaye kwasasa yupo Kenya kwa mkopo.
“Hata sisi tunaona hilo pengo la timu yetu kukosa mshambuliaji wa kati, lakini nikwambie tu watu husika kwa kazi ya kutafuta wachezaji wameanza kazi ya kutafuta mshambuliaji mkali mwenye uwezo mkubwa wa kufunga lakini pia tunamfuatilia Kiongera kwa kuwa bado ni mali yetu,”alisema Aveva.
“Kwasasa tunaye Sserunkuma (Danny) lakini tunakiri kwamba bado hajafanikiwa kutupa kile tulichokitarajia kutoka kwake katika hilo hatujakata tamaa soka ni mchezo wa subira kidogo tunaendelea kumpa muda kwa kuwa ligi bado atazoea tu.”
Akizungumzia majaliwa ya Kopunovic ambaye mkataba wake wa miezi sita wake unamalizika mwisho wa msimu huu, Aveva alisema kwasasa uongozi wake unaimani kubwa na kocha huyo baada ya kuitoa timu hiyo kutoka nafasi ya nane mpaka sasa ipo katika nafasi ya nne.
Alisema bado hajajua nini kitafanyika mwishoni mwa msimu ambapo kwasasa wanasubiri ripoti ya kamati ya ufundi.
“Tunafurahia kazi ya Kopunovic katika timu yetu tuseme ule ukweli ukiangalia aliikuta timu yetu katika nafasi ya nane ambayo haikuwa nafasi nzuri kulingana na ukubwa wa timu yetu na sasa tupo nafasi ya nne na tunaendelea kupambana.”
“Tunaendelea kumpa ushirikiano kwa kila analohitaji tunasubiri mambo mazuri zaidi katika mechi zilizosalia lakini kuhusu nini tutaamua mwisho wa msimu tunasubiri kwanza ripoti ya kamati ya ufundi baada ya ligi kumalizika.”

No comments