Simba yagundua uchawi wa Msuva




WAKATI Simba wakiweweseka na kasi ya mabao aliyonayo Simon Msuva wa Yanga, kinara huyo wa mabao wa Ligi Kuu ni kama amewafichulia siri yake.
Msuva mwenye mabao 11, matano kati ya hayo akiyafunga kwa kichwa, mawili kwa penalti na manne kwa mguu alifichua kuwa wala si uchawi kama watu wanavyofikiria bali ni ujanja wake wa kuiba muda wa kocha wake, Mholanzi Hans Pluijm wanapokuwa mazoezi ili kujifunza kufunga ndiyo sababu ya kumfunika Didier Kavumbagu mwenye mabao 10.
Aliweka wazi kuwa, amekuwa akiwasumbua, Juma Abdul na Mnyarwanda Mbuyu Twite mara kwa mara wampigie mipira ya krosi na yeye amalizie kufunga kwa kichwa au mguu huku makipa, Deogratius Munishi ‘Dida’ na Ally Mustapha ‘Barthez’ akiwaomba wakae golini.
Alisema, amekuwa akifanya hivyo karibu kila kipindi cha mazoezi na kila mmoja amekuwa anamwomba ampigie mipira mitano au sita na  kwa upande wa makipa mbali na kuokoa mipira hiyo ya krosi, huwa anawapigia mipira mingine mitano ya penalti kila mmoja.
Akizungumza na Mwanaspoti, Msuva alisema: “Ninatamani kufunga, napenda nifunge na hamu yangu ni kufunga lakini pale ninapoweza faida ya klabu na mimi mwenyewe, nikawa nafanya sana mazoezi ili nifanikiwe.”
“Nimekuwa nikiwasumbua sana baadhi ya wachezaji mazoezini, huwa naibia mwalimu anapokuwa amesimamisha programu yake kwa muda mfupi, huwa nawaomba wanipigie krosi na mimi nijaribu kufunga kwa kichwa na miguu makipa wakiwa golini. Wakati mwingine nawaomba pia wachezaji wa katikati wanichezeshee mipira nayo nafunga ni hivyo tu,” alisema Msuva ambaye amefunga mabao ya kichwa katika mechi waliyocheza na Prisons mzunguko wa kwanza bao moja, raundi ya pili mawili dhidi ya Prisons, moja na Mbeya City na moja dhidi ya Azam.
“Lakini pamoja na hamu yangu hiyo, huwa silazimishi kufanya hivyo, ninapokuwa sina uwezo, pia namwomba Mungu anilinde na majeraha ili nitimize malengo yangu ya kufunga kadri niwezavyo ili niwe mfungaji bora na timu yangu ichukue ubingwa.”
Msuva ambaye kuna habari kwamba Simba inamuwania pia aling’ara kwa mabao kwenye michuano ya Kombe la Mapinduzi ambalo hata hivyo ni mahasimu wao Simba ndio waliobeba taji la michuano hiyo.
REKODI
Awali Msuva alikuwa anacheza straika wa kati katika klabu mbalimbali alizopitia kama, Azam FC, Moro United na timu za Taifa za vijana chini ya miaka 17 na 20.
Baada ya kutua Yanga, alihamishiwa pembeni nafasi ya winga na yeye anasema: “Sina tatizo kucheza nafasi hiyo, kama una uwezo wa kufunga mabao, kokote utafunga iwe straika wa kati au winga pembeni.”
Kocha wake mkuu, Mholanzi Hans Pluijm amesifu kiwango cha Msuva kuwa ni mchezaji anayefuata maelekezo na kukubalia mabadiliko.

No comments