Adui wa Simba aanikwa live...




KOCHA Mkuu wa Simba amewatahadharisha wachezaji na viongozi wa Simba kwamba mechi yao ijayo dhidi ya Kagera Sugar ni kama vita kwani wakiteleza tu wameumia.
Goran Kopunovic alisema Kagera Sugar ndiyo adui wao mkubwa kwa sasa katika harakati zao za kumaliza pazuri katika Ligi Kuu.
Kopunovic raia wa Serbia alisema katika mazoezi yao yaliyoanza jana kuwa wanataka kujifua kwa nguvu kuhakikisha wanakwenda kuchukua pointi tatu dhidi ya timu hiyo watakayoumana nayo Jumamosi ijayo.
Alisema Kagera ndiyo adui wao mpya kutokana na kuwa chini yao katika msimamo wa Ligi Kuu kwani kama itapoteza mechi hiyo inaweza kuwa hatari kwao katika mbio za kuelekea juu.
Alisema katika kuyakimbia mazingira hayo anataka kutumia wiki moja kuwaandaa wachezaji wake kupambana katika Uwanja wa Kambarage Shinyanga ambao ulishawapa mazingira magumu kwa kufungwa na Stand United ya huko kwa bao 1-0.
“Kwa sasa Kagera ni adui katika safari yetu, tukifanya makosa tunaweza kuwa hatarini katika mbio zetu, nataka kuona Simba inashinda ndiyo maana nataka timu ianze mapema mazoezi,” alisema. “Ukiangalia msimamo utagundua tumewazidi mchezo mmoja, hatujui nini kitatokea katika mechi hiyo, endapo watashinda wanaweza kutukaribia zaidi. Kuwakimbia ni lazima tushinde, naujua sasa uwanja wao wa Shinyanga, najua nilipoteza pale lakini sasa najua cha kuifanya.” Katika hatua nyingine, Simba inakabiliwa na mchezo mgumu wa ugenini dhidi ya Kagera ikiwa hatarini kuwakosa nyota wake watatu. Nyota hao ni kipa Ivo Mapunda, beki Joseph Owino na winga Ramadhani Singano ‘Messi’ walio majeruhi. Hata hivyo, cha kufurahisha ni kwamba, beki wao Juuko Murshid aliyekuwa akiiwakilisha nchi yake ya Uganda katika pambano lao na Nigeria na kuibuka washindi wa bao 1-0, amerejea. wakati Emmanuel Okwi ana ruhusa maalumu kwenda kwao, lakini inadaiwa ataiwahi mechi na Kagera.
Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara alianika hayo jana: “Ivo, Singano na Owino ni majeruhi na Okwi yupo kwao Uganda na Murshid tunatarajia kumpokea akitoka kuwakilisha nchi yake,” alisema Manara.
Alidokeza timu itaondoka mapema wiki ijayo kuwahi pambano hilo.  Katika hatua nyingine, kundi la wanachama wa Simba linakwenda Zanzibar kwa ajili ya Michezo ya Pasaka wakiwa wageni wa Kikwajuni.

No comments