Twite amtokea kocha wa Yanga usiku wa manane



MHOLANZI pekee kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara anayeinoa Yanga, Hans Pluijm (66), ameushangaa uamuzi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kugoma kusogeza mbele mchezo wao dhidi ya Mtibwa wa Machi 8, lakini akasimulia maajabu mazito yanayomtokea akiwa usingizini kuhusu kiraka wake, Mbuyu Twite.
Pluijm ametamka kwamba katika hali isiyo ya kawaida, kuna wakati akiwa amelala usiku mnene inamjia sauti ikimwarifu kwamba beki huyo ni msaada mkubwa kwenye timu.
Alisema sauti hiyo imekuwa ikimtokea wakati beki huyo akiwa majeruhi na mara moja imewahi kumtokea akiwa na Yanga Misri wakati wakijiandaa kucheza na Al Ahly ya Misri msimu uliopita kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika walipotolewa kwa penalti.
Alisema pia usiku wa kabla ya mchezo wa juzi Jumatano dhidi ya Coastal Union mjini Tanga, aliisikia tena sauti hiyo na alipoamka siku ya mchezo akakuta mchezaji huyo yupo fiti na alipompanga akafanya kazi kubwa ya kuwazuia washambuliaji wa Coastal huku mpira wake wa kurusha ukizaa bao pekee lililoipa ushindi Yanga likifungwa na nahodha, Nadir Haroub ‘Cannavaro’.
“Sijui ni nini, lakini hayo ndiyo huwa yananitokea na nikija uwanjani utaona kweli Twite anakufanyia kazi yako vizuri, ni mpambanaji mzuri ambaye siku zote amekuwa hataki kufanya makosa,” alisema Pluijm ambaye alioa Oktoba 6, 1971.
“Nidhamu yake ya uwanjani haina tofauti kubwa na ile ya nje ya uwanja, hana tofauti kubwa na Cannavaro (Nadir Haroub) ambaye naye amekuwa mfano mzuri wa mabeki sio wa Yanga pekee hata wa timu nyingine,” aliongeza kocha huyo ambaye timu yake ilipoifunga Coastal shabiki maarufu wa Yanga, Ally Yanga, alipigwa jiwe katika paji ya uso na kupoteza fahamu. Ally ambaye hupenda kuvaa kitambi huku uso wake akipaka vumbi la mkaa alikutana na kasheshe hilo katika Uwanja wa Mkwakwani wakati akishangilia bao la Cannavaro na shabiki mmoja wa Coastal alimrushia jiwe hilo ambalo lilimpoteza fahamu kabla ya kuwahishwa hospitali.
Kichekesho ni pale ambapo Ally alirudiwa na fahamu na kutoroka hospitali alipoambiwa na muuguzi kwamba Yanga imeshinda.
“Viatu sijui viko wapi mimi nimetoroka pale hospitali, nilishangaa kujikuta nipo hospitali lakini nikauliza swali moja matokeo ya Yanga vipi, mhudumu akaniambia kwamba Yanga imeshinda bao lilelile moja akinitaka nitulie alipotoka nikasema hapa hapa naondoka,” alisimulia Ally huku waliokuwa karibu yake wakiangua vicheko.

No comments