Simba yaleta kocha mwingine.. Soma hapa


UKISIKIA ujanja wa mjini ndiyo huu. Ishu ipo hivi; Yanga kupitia kwa Mwanasheria wake, Frank Chacha, ilitangaza kuishtaki Simba kwa kitendo chake cha kuingilia usajili wa Emmanuel Okwi na kutaka ilipwe fidia ya Sh1.7 bilioni.
Simba imeweka wazi kwamba wala haina tatizo na itashiriki vizuri kutoa ushahidi wa kila kitu kuhusu madai hayo ya Yanga na wakishinda basi wao ndiyo watadai fidia hiyo kutoka kwa Yanga.
Mabosi wa Simba wakajikausha kama hawajasikia vile mkwara wa Yanga na kuendelea na mikakati yao ya kutwaa ubingwa wa Kombe la Mapinduzi na walipofanikiwa wakaigeukia Yanga na kutazama madai yao.
Katika madai yake ya msingi, Yanga ilisema itafungua kesi Shirikisho la Kimataifa la Vyama vya Soka (Fifa) kudai fidia kwa waliokuwa wachezaji wake; Okwi, Juma Kaseja na Genilson Santos ‘Jaja’ kwa kuvunja mikataba yao.
Kuhusu Okwi, Yanga inadai fidia ya Sh1.7 bilioni kwa Simba baada ya kumtumia huku ikijua kuwa ana mkataba na klabu hiyo ya Jangwani pia ikaihusisha timu ya Delga ya Misri ambayo ilifanya mazungumzo na mchezaji huyo isivyo halali.
Kwa upande wake, Kaseja anadaiwa fidia ya Sh300 milioni kwa kitendo chake cha kutoonekana kazini na kuvunja mkataba akiwa amelipwa haki zake zote wakati Jaja anadaiwa fidia ya Sh95 milioni kwa kuvunja mkataba baada ya kushindwa kurejea nchini alipoenda mapumzikoni kwao Brazil Novemba mwaka jana.
Baada ya kutafakari kwa kina madai hayo ya Yanga, Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Poppe alisema watani wao wa jadi wanaonekana kutapatapa nje ya uwanja na watasikiliza kesi yao ya madai na (Yanga) wakishindwa itabidi wao ndiyo walipe fidia hiyo kwa usumbufu.
“Yanga wanadai fidia ya Sh1.7 bilioni, mbona wanaonekana kama wanatapatapa? Nadhani wameishiwa fedha sasa, hawa wanaonyesha ishara ya kufilisika ndiyo maana wana madai mengi yasiyo na maana,” alisema Han Poppe ambaye ni Mwenyekiti wa Kundi la Friends of Simba.
“Waache waende Fifa, sisi tutasikiliza madai yao na tutatoa ushahidi wetu kuhusu kila kitu cha Okwi na Yanga wakishindwa kesi hiyo basi wajiandae kuilipa Simba kiasi kama hicho cha fedha.”
Yaleta kocha mwingine
Siku chache baada ya kutwaa Kombe la Mapinduzi, Simba inamleta kocha wa makipa wake na tayari ina mapendekezo ya makocha wawili mmoja kutoka Kenya, Idd Mohamed Salim na mwingine kutoka Uganda.
Lakini kabla ya kumalizana na mmoja kati ya hao, huenda makipa wa Simba wakafundishwa kwa muda na kocha Choki Abeid kutoka Oman.

No comments