Simba hii ya sasa ni ya kuogopwa




ACHANA na ubingwa wa Kombe la Mapinduzi ilioutwaa Jumanne usiku kwa kuifunga Mtibwa Sugar penalti 4-3, Simba ya sasa ni ya kuogopwa na ina kiburi.
Saa chache tu baada ya kutwaa taji hilo, kocha wa timu hiyo, Goran Kopunovic, amewataka wachezaji wake kusahau kabisa kuhusu walichofanya katika michuano hiyo na amewataka moto huo wauhamishie katika Ligi Kuu Bara.
Kocha huyo Mserbia mwenye ufahamu mkubwa wa soka la Afrika akiwa amewahi kuifundisha Polisi Rwanda, amewaambia wachezaji wake kuwa timu watakazokutana nazo katika ligi lazima zionje makali ya vipigo kutoka kwao ili kuthibitisha ubora wao.
Katika msimamo wa ligi, Simba inashika nafasi ya 12 kati ya timu 14 ikiwa na pointi tisa tu baada ya kucheza mechi nane.
Keshokutwa Jumamosi timu hiyo itacheza na Ndanda FC ya Mtwara ambayo ipo nafasi ya 11 ikiwa na pointi 10 baada ya kucheza mechi kumi. Mechi hiyo itachezwa kwenye Uwanja wa Nangwanda Sijaona mjini Mtwara.
Mapema jana Jumatano Kopunovic aliwasili Dar es Salaam akiwa na kikosi chake wakitokea Unguja na kombe lao walilotwaa na walitumia saa chache kwa mapumziko na mchana wakaenda Mtwara kujiandaa na mechi dhidi ya Ndanda.
“Nashukuru tumefanikiwa kutwaa Kombe la Mapinduzi, si taji kubwa sana, lakini imekuwa ni fursa ya kukijenga kikosi chetu, nafurahi kuona timu imekamilika kila idara, tutafanya vizuri kwenye ligi,” alisema.
“Nataka hamasa tuliyotoka nayo huku kwenye Mapinduzi itupe nguvu ya kufanya vizuri kwenye ligi, morali ya juu ya wachezaji inanipa nguvu na matumaini ya kufanya vyema hasa katika mchezo wetu wa wikiendi (dhidi ya Ndanda).
“Unajua nimeambiwa Simba ilikuwa haipati matokeo mazuri huku kila timu ikijitahidi kutoka nayo sare, nafikiri sasa mambo yamebadilika na wanapaswa kutuogopa kwani tuna morali ya ubingwa na wachezaji wangu wametulia na kufuata maelekezo vizuri.”
Kocha huyo anayeamini katika soka la kasi na pasi za kuachiana haraka haraka, aliliambia Mwanaspoti kuwa kwa jinsi kikosi chake kilivyo sasa, haoni timu itakayowasumbua tofauti ilivyokuwa mwanzo kabla hajafika.
Okwi apiga mkwara
Straika Emmanuel Okwi naye amesema haoni sababu ya kikosi chao kuendelea kupata matokeo mabaya kwenye mechi za ligi kwani sasa kipo vizuri na ari ya kupambana kwa wachezaji wote kwenye timu iko juu.

No comments