Okwi ampagawisha Mserbia



FOWADI wa Simba ambaye mashabiki walikuwa wakimmaindi kwa madai kwamba ni msumbufu, Emmanuel Okwi, ametua kambini kwa mbwembwe na kufanya mambo ya maana ambayo yamemzingua na kumpagawisha kocha Mserbia, Goran Kopunovic.
Lakini siyo hilo tu, Okwi ambaye alijiunga na Simba akitokea Yanga amelitumia Mwanaspoti kutoa ufafanuzi wa kina kwa mashabiki wa Simba kuhusiana na hali yake ya kuchelewa kuripoti pamoja na mchakato wake wa harusi.
Kopunovic anayependa kufundisha vitu kwa vitendo zaidi, alimpokea Okwi juzi Jumamosi mchana lakini katika muda mfupi aliokaa naye akafanya mambo ambayo yalimshtua kidogo na kumfanya kocha huyo akubali kwamba jamaa ni bonge la mchezaji tofauti na alivyokuwa akisikia.
Kopunovic alisema amefurahishwa na kuwasili kwa Okwi katika timu hiyo lakini kubwa lililomvutia zaidi ni vile mchezaji huyo alivyotumia akili ya kuzaliwa kupandisha morali ya wachezaji wenzake akiwataka kufanya kweli katika mchezo wa nusu fainali ambao Simba iliichapa Polisi bao 1-0.
Bosi huyo alisema tofauti na alivyomtarajia, Okwi alitumia muda mwingi kuwahamasisha wenzie kucheza kufa kupona ili awepo katika fainali dhidi ya Mtibwa itakayopigwa kesho Jumanne usiku kwenye Uwanja wa Amaan na kurushwa ‘Live’ na Azam TV.
Kopunovic alisema Okwi ameonyesha kitendo cha kiungwana sana na atajaribu kukaa naye chini kujadiliana mambo ya maana zaidi kikazi ikiwemo mbinu za kuimaliza Mtibwa Sugar ambayo imekuwa ikiitesa Simba hivi karibuni.
“Ni mchezaji muhimu Simba, nimegundua hilo katika muda mfupi aliokaa hapa, anajua afanye nini, angalia alivyobadilisha morali ya wachezaji wenzake aliwapa maneno ambayo thamani yake ni matokeo ya mechi ya nusu fainali,” alisema Kopunovic. “Nataka kufanya kazi na wachezaji wenye akili kama hiyo, naamini mchezo ujao atakuwa uwanjani.”
Kuhusu kuoa na ruhusa
“Nasikia tu kwamba nimekwenda kuoa mara nipo kwenye fungate hakuna ukweli wowote mimi sijaoa bado kama inavyodaiwa, ndoa halisi ni Julai nikitulia, hapa nilikuwa namsogeza tu mwenzangu nyumbani,” alisema Okwi.
“Unajua kule kwetu Uganda wakati wa kuchumbia kama nilivyofanya, ndiyo huwa muda wa hiyo sherehe fupi. Ni kama tunafanya utambulisho tu.”
Okwi alisema aliomba muda wa kumpuzika kidogo, lakini wakati anaondoka hakuambiwa anatakiwa arudi lini.
Okwi alisema anatambua majukumu yake ndani ya Simba ambapo alikuwa anaifuatilia timu hiyo kila hatua na sasa amerudi rasmi kuanza kazi.

No comments