Huyu ndiye aliyekuwa kiboko ya Simba.. Legendary




KATIKA toleo la Jumanne iliyopita, mshambuliaji wa zamani wa Yanga aliyekuwa kiboko ya Simba, Said Sued ‘Scud’ alizungumzia jinsi alivyoondoka katika klabu hiyo baada ya msimu mmoja wa mafanikio. Endelea…
Unaweza kushangaa kwani licha ya kufanya maajabu kwa kuifunga Simba mara mbili katika msimu mmoja, Scud alichezea Yanga kwa msimu huo mmoja tu, ulipomalizika alikwenda kuichezea Milambo ya Tabora aliyodumu nayo kwa miaka mitano.
Habari zilizotawala wakati huo ni kwamba Scud alikuwa mwenye maringo hasa baada ya kuifunga Simba mara mbili, rekodi yake hiyo ya kuvutia ilimpa heshima ya kipekee mbele ya mashabiki wa Yanga.
Hali hiyo ilitokana na ukweli kwamba enzi hizo mechi za Yanga na Simba zilikuwa na mvuto wa kipekee, ilikuwa ni Simba na Yanga hasa. Lakini Scud anasemaje kuhusu kuondoka kwake Yanga.
“Kila kitu huwa naamini ni mipango ya Mungu na siwezi kumlaumu yeyote kutokana na jambo hilo,”anasema Scud.
Scud anasema, anachokumbuka baada ya ligi kumalizika alikwenda kwa bosi wake anamtaja kwa jina la Ramesh Patwa ili apewe tiketi ya ndege ya kurudi kwao Kigoma.
Alipewa tiketi kama kawaida na fomu ya usajili ili aijaze kwa ajili ya msimu ujao akaipokea, hata hivyo alishapewa taarifa, alikuwa kwenye mpango wa kusajiliwa na kuachwa kwa kile kilichodaiwa kuwa alikuwa na maringo.
“Nilipotoka nje nilikutana na Abbas Mchemba na Dadi Fares wote walikuwa wachezaji wa African Sports ya Tanga na kuniambia kuwa wanakwenda Tabora kusajili Milambo, tuliachana hapo mimi nikaelekea nyumbani,” anasema Scud ambaye ni kaka wa kuzaliwa wa mshambuliaji wa Coastal Union, Hussein Sued.
“Wakati huo niko na fomu yangu, lakini kumbe wale wachezaji niliokutana nao Dadi na Mchemba walipeleka taarifa Milambo ambayo ilimtuma mchezaji wao wa zamani Wastara Baribari anifuate Kigoma. Tulizungumza na kukubaliana ndipo nikaenda Milambo na kusajiliwa rasmi,”anaeleza Scud na kuwataja aliosajiliwa nao kuwa ni Jobe Ayoub, Said John na huo ukawa mwisho wake Yanga.
Anasema, hapo alicheza misimu mitano na baada ya hapo, alirudi kwao Kigoma na kusajiliwa na National sasa ni Mbanga FC iliyokuwa Daraja la Pili.
Akizungumzia sababu ya kustaafu soka anasema kuwa aliamua tu: “Sikupatwa na majeraha yoyote hadi kustaafu, niliamua mwenyewe tu.”
Baada ya mazungumzo hayo mwandishi alimshawishi Scud amtembeze zizini kwenye mifugo yake na kujionea kilichokuwepo, naye bila kusita alifanya hivyo.

No comments