Habari kutoka Yanga




SIMBA na Yanga zimerudi na mkwara mzito kwenye Ligi Kuu Bara ambapo zimeikejeli Mtibwa Sugar kwa kuiambia kwamba sasa ndio ngoma ya kikubwa inaanza.
Mtibwa imekaa kileleni mwa msimamo wa Ligi tangu mwanzoni mwa msimu na imekuwa ikizitesa Simba na Yanga ambazo zimedai kwamba zilikuwa zinausoma mchezo kwenye mechi za awali.
Timu hizo kongwe nchini ambazo zimeonekana kuzidiwa maarifa ya uwanjani na Mtibwa, kila moja kupitia kwa makocha wake raia wa kigeni imesisitiza kwamba sasa inafungua ukurasa mpya na ligi ndiyo imeanza kwao, huku kiburi cha kutwaa Kombe la Mapinduzi mbele ya Mtibwa kikiivimbisha kichwa Simba ambayo ilishinda mechi moja tu kati ya nane za mwanzo ilizocheza kwenye ligi.
Wanachama matajiri wa Simba ambao walikuwa karibu na timu hiyo kwenye Kombe la Mapinduzi, wamerejesha nguvu zao kwenye Ligi Kuu na wikiendi hii wametapakaa Mtwara kuhakikisha timuj hiyo inarejea kwenye nafasi mbili za juu kwa kuhamasisha wachezaji washinde kwa nguvu zote.
Simba imesafiri kwenda Mtwara kucheza na Ndanda FC ya mjini humo. Itakuwa mechi ya kwanza ya ligi kwa kocha Goran Kopunovic aliyechukua mikoba ya Patrick Phiri mapema mwaka huu.
Yanga wao  watakuwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuikabili Ruvu Shooting ya Pwani, ikiwa ni mechi ya pili ya ligi kwa Hans Pluijm aliyechukua mikoba ya Marcio Maximo mwishoni mwa mwaka jana.
Yanga v Ruvu
Yanga baada ya kutolewa mapema kwenye michuano ya Mapinduzi iliweka kambi ya wiki nzima Bagamoyo, Pwani kujiandaa na mchezo huo wa Ruvu ambapo kocha wa timu hiyo, Pluijm, alikuwa akiwasisitiza wachezaji wake  kuwa makini katika kufunga na kucheza kwa kasi bila kutoa nafasi kwa adui.
 Yanga inashika nafasi ya tatu kwenye ligi ikiwa na pointi 14 wakati Ruvu wao wanashika nafasi ya tisa na pointi zao 11.
Katika mazoezi ya timu hiyo yaliyokuwa yakiendelea kwenye Uwanja wa Boko Veterani nje kidogo ya Dar, Pluijm alitumia muda mwingi katika upigaji wa mashuti katika staili mbalimbali huku akisisitiza mpira wa kasi na kuziba nafasi zinazoweza kutumiwa na maadui wao.
Pluijm alisema: “Tunataka kushinda, hivyo lazima tutumie mbinu mbalimbali, nataka timu icheze kwa kasi, lakini wasitoe nafasi kwa adui na ndiyo maana tunaubana uwanja ndogo wakati wa mazoezi. Ruvu wanatumia nguvu na wanakaba zaidi na kushambulia kwa kushtukiza na ndiyo maana nataka timu icheze kwa kasi na kuziba mashambulizi yao.”
Yanga itamkosa beki Nadir Haroub ‘Cannavaro’ anayetumikia adhabu ya kadi nyekundu. Kiraka Mbuyu Twite naye huenda akaukosa mchezo huo kutokana na majeraha ya goti lakini beki Rajab Zahir tayari ameandaliwa kuziba nafasi hiyo.

No comments