Yanga yasainisha mwingine

Tambwe akitia dole gumba kwenye mkataba wa usajili dhidi ya timu ya Yanga ya jijini Dar es Salaam, kushoto ni wakili Stoki Joachim

UONGOZI wa Yanga, umefanya uamuzi mgumu baada ya kumpiga chini kocha wao, Marcio Maximo na kiungo Mbrazili, Emerson Rouqe (pichani) sambamba na kumsainisha straika aliyeachwa na Simba, Amissi Tambwe.
Yanga imefikia hatua hiyo jana Jumatatu katika dakika za mwisho za usajili wa Ligi Kuu Bara na sasa Mholanzi, Hans Pluijm anarudi Jangwani kuziba nafasi ya Maximo akisaidiwa na Boniface Mkwasa.
Mwanaspoti imethibisha kwamba Tambwe aliyekuwa mfungaji bora msimu uliopita alisaini mkataba wa mwaka mmoja na Yanga mbele mmoja wa vigogo wazito wa Jangwani, Francis Kifukwe na mwanasheria wa klabu.
Habari za uhakika zinasema kwamba Yanga wameamua kumtema Maximo baada ya kocha huyo kushikilia misimamo yake kwa kugoma kumtema msaidizi wake, Leonardo Neiva ili nafasi yake ichukuliwe na Mkwasa.
Uongozi wa Yanga ulitaka Mkwasa amuongezee nguvu Maximo kwa maelezo kwamba timu imemzidi nguvu na anahitaji msaidizi mzalendo lakini Maximo akagoma na kuwaambia kwamba leo Jumanne atawapa msimamo wake ambao ni kujiuzulu.
Habari za uhakika ni kwamba Yanga wameafikiana kumtema kiungo, Emerson ambaye usajili wake ulikuwa haujakamilika na kubakiwa na Mbrazili, Andrey Coutinho ambaye ana mkataba mrefu.
Imeelezwa kwamba Yanga hawakubaliani na kiburi cha kocha huyo hasa kwa kumtema Hamis Kiiza na kuwabakisha Wabrazili wenzake.
Hatua hiyo ya Yanga imetokana na ushindi mdogo inayopata timu hiyo katika mechi za hivi karibuni, usajili wa gharama ambao hauonyeshi dalili ya kuleta matunda pamoja na kipigo cha mabao 2-0 ilichopata dhidi ya Simba kwenye mechi ya Nani Mtani Jembe.
Mabosi hao wa Yanga ambao walikutana jijini Dar es Salaam juzi na jana wanamtaja mdachi Hans Pluijm kama mrithi wa Maximo aliyetua nchini Juni 26, mwaka huu na kupokelewa kwa mbwembwe Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere, Dar es Salaam.
“Hataki kutusikiliza kila mtu ameona kwamba Coutinho hana uwezo wa kutosha kulingana na Kiiza tukamshauri basi kama Kiiza hamtaki tumuondoe Coutinho ili nafasi yake tutafute mchezaji ambaye ataisaidia timu zaidi yake lakini amekuwa hakubaliani na hilo akisisitiza kwamba bado anamuhitaji,”alisema mmoja wa mabosi wa Yanga ingawa aliongeza kwamba baadaye viongozi walikuja kukubaliana kwamba abaki Coutinho na aondoke Emerson.
“Tunaachana naye ili atuachie timu yetu, kadiri muda unavyozidi kwenda uwezo wa timu umekuwa ukipungua taratibu, Yanga imekuwa ikishinda kwa kubahatisha sana kitu ambacho huko nyuma hakikuwepo,”aliongeza kigogo huyo na kudai kuwa kuna kigogo mmoja mzito ndani ya Yanga anamkingia kifua Maximo.
Katika mpango huo wa kumuondoa Maximo anayechukua mshahara wa dola 12000 (Sh 20.8ml) kwa mwezi tayari Mwanaspoti lina taarifa kwamba Yanga ipo katika hatua za kumrudisha Pluijm ambaye sasa hana kazi.

No comments