Mliberia amuumbua mtu

 
Mliberia wa Yanga, Kpah Sherman 

NI kama amemuumbua lakini amemtumia kufikisha ujumbe kwa mashabiki na timu pinzani kwamba yeye ni straika mkali. Mliberia wa Yanga, Kpah Sherman jana amempiga Ally Mustapha ‘Barthez’ hat trick mazoezini.
Katika mazoezi hayo ya jana Jumatatu asubuhi kwenye Uwanja wa Shule ya Sekondari Loyola, Kocha wa Yanga, Marcio Maximo alitumia muda mrefu kuwaelekeza mabeki wake jinsi ya kuokoa mipira kutoka pembeni hasa ya juu.
Wakati wote wa mazoezi hayo, langoni alikuwa kipa namba mbili Ally Mustapha ‘Barthez’ ambaye alionekana kuwa makini akisaidiana na mabeki wa kati Nadir Haroub ‘Cannavaro’ na Kelvin Yondani.
Zoezi hilo lilihusisha mipira ya krosi ambayo Yanga ilionekana kutokuwa makini kuokoa katika mchezo wao dhidi ya Simba wikiendi iliyopita ambao uliisha kwa Simba kushinda mabao 2-0.
Mazoezi hayo yalihamia kwa washambuliaji wa timu hiyo kupewa mbinu za kufunga kwa kutumia mipira hiyo ya krosi ambao walioonekana kuwekewa mkazo ni beki Cannavaro na straika Mliberia Kpah Sherman.
Sherman, ambaye mashabiki wa Yanga wamemkubali kwa roho moja kutokana na uwezo wake, alimfundisha soka Barthez na kumpa mambo ambayo yamemtofautisha na mastraika wengine, alimfunga mabao matatu yaliyoenda shule. Straika huyo amechukua nafasi ya Hamis Kiiza wa Uganda aliyeachwa na Marcio Maximo.
Katika mechi ya kirafiki ya Nani Mtani Jembe, Yanga ilifungwa bao la pili na Elius Maguli baada ya mabeki wake kutokuwa makini kuokoa mpira wa kurushwa kutoka upande wa kulia, hivyo Maximo ametaka kuhakikisha makosa hayo hayatokei tena. Yanga ililala mabao 2-0 dhidi ya Simba.
SHERMAN ANENA
“Ninachotazama sasa nikuhakikisha najituma zaidi ili Yanga ipate mafanikio, nimeona ipo nafasi ya pili katika msimamo na idadi ya mechi inalingana na timu zote, nawahakikishia mashabiki wa Yanga kuwa kuna uwezekano mkubwa wa kutwaa ubingwa kwani tuna timu nzuri ya ushindani,” alisema Sherman.
Hata hivyo Sherman aliyesajiliwa na Yanga kutoka klabu ya Centikaya ya Cyprus alilazimika kutoka baada ya kuumia dakika ya 62 na nafasi yake akaingia Mrisho Ngassa.
“Mchezo wa Simba umenifanya nihisi nina kazi ya kufanya na naamini nitaweza kuipa matunda Yanga kwani najiamini naweza, idadi ya mashabiki ilinishangaza kwa kweli,” alisema Sherman

No comments