Straika Yanga atoa siri za Kocha mpya wa Simba. Soma hapa



MTAIPENDA hii kwani imekaa vizuri. Kocha mpya wa Simba, Goran Kopunovic, ameshaanza kazi pale Msimbazi lakini straika wa Yanga, Danny Mrwanda amewaambia wenzake: “Tulieni najua kila kitu chake, hawezi kutusumbua.”
Kopunovic na Mrwanda walikutana Vietnam katika klabu ya Dong Tam Long An na walifanya kazi pamoja kwa muda kidogo kabla ya straika huyo kuhamia timu nyingine, Hoang Anh Gia Lai.
Akizungumza na Mwanaspoti, Mrwanda alisema amefurahi kukutana tena na kocha wake huyo wa zamani hata kama sasa wapo timu tofauti na amemtaka bosi wake wa Yanga, Hans Van Der Pluijm na wachezaji wenzake kutokuwa na wasiwasi kuhusu Kopunovic.
Mrwanda alisema Kopunovic ni kocha mzuri na siku zote amekuwa anapenda kuona kikosi chake kikitengeneza mashambulizi makali kupitia viungo wa pembeni ambao huwaagiza kupiga krosi za kutosha kwa washambuliaji wa kati.
Straika huyo ambaye amewahi kuichezea Simba, alisema Kopunovic mbali na hilo anapenda kuona kikosi chake kikishambulia kwa kasi huku mashambulizi yakianzia kwa mabeki ambao hawatakiwi kukaa na mpira muda mwingi na kutakiwa kuuachia haraka kwa viungo au mabeki wa pembeni ambao nao jukumu lao ni kuwatafuta viungo wa pembeni yaani mawinga.
“Unajua mimi sioni kama kuna hatari katika timu yetu kuhusu ujio wa Goran (Kopunovic), tuna timu ambayo inaweza kupambana kutokana na uzoefu na kocha mwenye uwezo mkubwa wa kuwasoma wapinzani wake,” alisema Mrwanda.
“Nitamweleza Pluijm kuwa siku zote Kopunovic ni kocha anayependa timu yake kutumia mawinga na hata viungo wa kati kutengeneza mashambulizi sasa mkikutana na timu yake na mkafanikiwa kuwabana katika maeneo hayo uwezekano wa kumshinda mnao.
“Tulivyokuwa naye alikuwa anawazuia kabisa mabeki kukaa na mpira amekuwa akitaka wauachie haraka na kuwapa aidha mabeki wa pembeni au viungo wa kati ambao nao jukumu lao ni kupeleka mbele kwa mawinga, soka analopenda ni la kasi kidogo,” alisema Mrwanda.
Kopunovic aliyesaini mkataba wa miezi sita, alitarajiwa kuanza kazi jana Alhamisi kwa kuiongoza Simba katika mchezo wa Kombe la Mapinduzi dhidi ya Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Amaan, Zanzibar

No comments