
KWELI mambo ni kizungumkuti kwani Simba imempa mkataba wa miezi
sita Kocha Goran Kopunovic na hapo hapo imempa ‘likizo’ Patrick Phiri
aende kwao Zambia akapumzike.
Kopunovic raia wa Serbia amekubali kusaini mkataba
huo ambapo analipwa dola 3000 kwa mwezi (Sh5 milioni) wakati Phiri
alikuwa analipwa dola 2000 (Sh3.3 milioni) tofauti kati yao ikiwa ni
dola 1000 (Sh1.7 milioni).
Phiri amesitishiwa mkataba wake ‘kiaina’ baada ya
timu hiyo kutokuwa na matokeo mazuri katika mechi nane za Ligi Kuu Bara
ikishika nafasi ya kumi na pointi zake tisa. Simba imetoka sare sita,
imeshinda mechi moja na kufungwa mara moja.
Kwa siri uongozi wa Simba ukafanya mazungumzo
haraka na Kopunovic ili aje kuinusuru timu yao ambao kocha huyo
aliwasili nchini juzi Jumatano asubuhi kisha kufanya mazungumzo na
matajiri wa timu hiyo ambao jana walimpa mkataba wa miezi sita.
Kocha alitarajiwa kwenda Zanzibar muda wowote
baada ya kusaini mkataba huo kuiongoza Simba dhidi ya Mtibwa Sugar
katika Kombe la Mapinduzi kwenye Uwanja wa Amaan.
Kopunovic amekubali kufanya kazi hiyo kwa mshahara
huo unaoonekana kiduchu baada ya kujiridhisha na mazingira ya timu
anayojiunga nayo. Aliyekuwa Kocha wa Simba, Mserbia Dravko Logarusic
alikuwa analipwa dola 5000 (Sh8 milioni).
“Unajua Waserbia huwa hawachukui fedha nyingi
sana, lakini hii yote inategemea na makubaliano ya fedha wakati wa
kusaini mkataba, Phiri alichukuwa fedha nyingi katika kusaini mkataba
kuliko huyu ndiyo maana mishahara ipo tofauti,” alisema mmoja wa
viongozi wa Simba.
FIDIA YA PHIRI
Ni wazi Simba sasa inamtafuta mtu maalumu wa
kumpasulia ukweli Phiri kwamba hawatakuwa naye tena, lakini klabu hiyo
italazimika kumlipa kocha huyo dola 8000 (Sh13.5 milioni) za fidia na
malipo ya mishahara yake ya miezi mitatu ambayo hakulipwa.
Kwa mujibu wa mkataba wa Phiri na Simba, yeyote
atakayevunja mkataba anatakiwa kumlipa mwenzake mshahara wa mwezi mmoja.
Akizungumza na Mwanaspoti, Phiri alisema; “Maisha ya soka ndivyo
yalivyo na unatakiwa kujiandaa kwa lolote na muda wowote, wamemleta
kocha bila kuniambia lolote na nilipowauliza kuhusu hali hiyo wamekataa,
ndiyo maana nimewaambia niende nyumbani kwa mapumziko mafupi na
wamekubali.
“Mambo ya kufukuza kocha siyo ya kufichana kwani
mimi siyo lazima niifundishe Simba, Aveva (Evan, Rais wa Simba) ni
rafiki yangu na ndiye alinipigia simu nikiwa Zambia kuniomba nije hapa
iweje sasa ashindwe kuniambia kama alivyofanya hapo awali.
“Naamini haki zangu watanilipa na hata kama
wakiamua kutonilipa nitahesabia kama nimepoteza kwa bahati mbaya, pia
nitamshukuru Mungu,” alisema Phiri. “Nitaondoka kesho (leo) labda
nikifika Zambia au wakati wa kuondoka ndiyo nitaambiwa rasmi, ila
namtakia kila la kheri kocha mpya aiwezeshe Simba kupata matokeo
mazuri.”
Post a Comment