Emmanuel Okwi ni noma





KOCHA mpya wa Simba, Goran Kopunovic ameanza kazi ya kukinoa kikosi cha timu yake visiwani Zanzibar huku akitakiwa kuwa makini na msimamo juu ya usumbufu wa mshambuliaji Emmanuel Okwi vinginevyo ataharibikiwa mapema tu.
Aliyetamka maneno hayo si mwingine bali ni Patrick Phiri kocha aliyesitishiwa mkataba wake na kuondoka nchini jana Ijumaa asubuhi kurudi kwao Zambia ambaye amemtakia kila la kheri Kopunovic katika kazi yake.
Akizungumza na Mwanaspoti katika mahojiano maalumu yaliyofanyika saa chache kabla ya kuondoka kwake, Phiri alisema kuwa katika kikosi cha Simba alichokaa nacho kwa miezi mitano hakuna mchezaji msumbufu kama Okwi lakini viongozi wanafumbia macho usumbufu wake.
“Okwi ni msumbufu sana na huyu kocha mpya (Goran) kama atakuwa mpole atamsumbua sana, sijawahi kuona mchezaji wa kimataifa msumbufu kama Okwi akienda kwao anarudi siku moja au mbili kabla ya mechi na viongozi hawasemi lolote.
“Kocha asikubali tabia hii ya Okwi iendelee ndani ya timu, binafsi sijakaa naye muda mwingi lakini ndiyo hivyo huwezi kusema lolote kwa viongozi juu ya Okwi wakakuelewa, Okwi ni mchezaji mzuri sana ila tabia zake kama hizi ndizo zinazokera na zitamrudisha nyuma,” alisema Phiri.
Phiri alimtaka mchezaji huyo kulinda kipaji chake kwa kujituma na kuwa na nidhamu ndani ya timu.
“Nidhamu haifundishwi na mtu ni jinsi mtu mwenyewe anavyoishi na kutaka kuwa hivyo, Okwi ana kipaji kikubwa lakini anaweza kukishusha mwenyewe kwa tabia zake, namshauri atulie acheze mpira atafanikiwa zaidi kwani Simba wanampa kila kitu afanye kazi iliyomleta,”.
Kwa sasa Okwi ameaga kwenda kwao Uganda kumalizia fungate baada ya kufunga ndoa hivi karibuni, lakini hadi juzi Alhamisi jioni alikuwepo Dar es Salaam. Mchezaji huyo ana ruhusa hiyo wakati timu ipo visiwani Zanzibar inakoshiriki Kombe la Mapinduzi.

No comments