Okwi aanzisha operesheni maalumu Msimbazi



KOCHA wa Simba, Mserbia Goran Kopunovic na kipa wake, Ivo Mapunda, wamempigia saluti straika wao, Emmanuel Okwi raia wa Uganda ambaye ndani ya dakika 180 za michezo miwili waliyocheza, amekuwa akifunga mabao ya staili moja kwa umbali wa zaidi ya mita 30 pembeni mwa uwanja.
Lakini Okwi amesisitiza kwamba sasa wachezaji wameanzisha operesheni maalum ambayo ubingwa haupo akili mwao kabisa, wanapiga moja moja baadaye kitaeleweka tu.
“Tunaweka kando suala la ubingwa na tunachotakiwa kufanya ni kushinda kila mechi halafu baadaye ndiyo itajulikana,” alisema.
Mganda huyo ameongeza kusema huwa hakosei kwa sababu amekuwa akiyafanyia kazi mara kwa mara anapokuwa mazoezini. Okwi amefunga mabao hayo mfululizo kwenye mechi yao na Yanga waliyoshinda 1-0 alifunga umbali wa mita 30 na juzi Jumamosi aliwafunga Mtibwa bao 1-0 umbali wa mita 35.
Mabao ambayo yamewapa raha mashabiki wa Simba ambao baada ya mechi, wamekuwa wakikusanyika nje ya uwanja na kuiimba “Okwi, Okwi.”
Akizungumza na Mwanaspoti, Okwi alisema: “Nimekuwa nafunga mabao ya aina hiyo kwa sababu huwa ninayafanyia kazi mara nyingi ninapokuwa mazoezini ndiyo maana inakuwa rahisi kwangu kufunga. Kama hili la Mtibwa, dakika zilivyokuwa zimekwisha, wakajua mechi imemalizika wakajisahau, mimi nikamwangalia kipa alivyokaa nikafunga.”
Okwi ambaye alitoka uwanjani Jumamosi akiwa amejaa noti alizozawadiwa na mashabiki, aliongeza: “Lakini kingine mbali na mazoezi, wachezaji ninaocheza nao, wananipa ushirikiano mzuri na ndiyo maana tunafanikiwa.”
Golan alisema ana kila sababu ya kumsifu Okwi kutokana na kiwango chake anachokionyesha uwanjani. Okwi aliwafunga Yanga kipa akiwa Ally Mustapha ‘Barthez’ na alipowafunga Mtibwa, mlinda mlango alikuwa, Said Mohamed. Mabao hayo yamewaweka matatani makipa hao.

No comments